Sh100 kuwapatia wanafunzi 27 ufadhili wa masomo
Washindi 10 wa shule ya sekondari katika picha ya pamoja na viongozi wa shule mbalimbali baada ya kukabidhiwa vyeti vya ushindi wa shindano la mitihani.
Muktasari:
Mashindano hayo yaliyohusisha Mitihani ya kimasomo zaidi ya wanafunzi 150 wa shule ya msingi na sekondari walishiriki kutoka shule 10 za kimataifa, Kati yao 27 wamefanikiwa kupata ufadhili wa masomo kwa punguzo la asilimia 50 hadi 75 ya ada kwa mwaka mpya wa masomo 2024 wenye thamani ya shilingi milioni 100.
Arusha. Jumla ya wanafunzi 27 nchini wamefanikiwa kupata ufadhili wa masomo baada ya kuibuka washindi kwenye shindano la mitihani ya kielimu iliyoanza mwezi Agosti hadi Septemba mwaka huu jijini Arusha.
Mashindano hayo yaliyohusisha zaidi ya wanafunzi 150 wa shule ya msingi na sekondari kutoka shule 10 za kimataifa, 27 wamefanikiwa kupata ufadhili huo kwa punguzo la asilimia 50 hadi 75 ya ada kwa mwaka mpya wa masomo 2024 wenye thamani ya Sh100 milioni.
Akizungumza katika hafla ya kuwakabidhi washindi vyeti na hati ya punguzo la ada, Mkurugenzi wa Shule ya kimataifa ya Meru, Dk Zeeshan Ahmed Khan alisema shindano hilo linalenga kutambua vipaji vya watoto vya kielimu hasa katika kuchangamsha ubongo wa kujibu maswali ya masomo wanayofundishwa na yanayotokea katika maisha.
"Shule ya kimataifa ya Arusha, Meru tumeamua kuanzisha shindano hili la kila mwaka la mitihani tuliyoiita 'Talent Hunt Scholarship 2023' ili kukuza ubora wa kitaaluma, kuthamini vipaji vya kielimu kwa watoto wetu lakini zaidi kuwapa changamoto ya ubongo mara kwa mara ili kuwekeza akili na mda wao mwingi katika masomo," alisema Zeeshan.
Zeeshan lisema miongoni mwa shule shiriki ni pamoja na Saint Constantine International, Braeburn School, Jaffery Academy, Arusha Meru, Prime School na (AMIS).
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, mmoja wa washindi hao, Pendo Karungu kutoka Shule ya Prime School alisema ufadhili huo utawapunguzia wazazi kwa kiasi kikubwa mzigo wa kifedha kwa ajili ya ada na kuwawezesha kufanya vyema kitaaluma.
"Mitihani ilikuwa migumu na yenye changamoto hasa kutokana na baadhi ya masomo hatujayafikia au tuliyapita kitambo lakini nina furaha kuwa nimeshinda na kusaidia kupunguza mzigo wa karo za shule kwa wazazi wangu," alisema.
Mmoja wa wazazi hao, Sabrina Roshan alisema shindano hilo la kusaka vipaji vinasaidia watoto kujituma kimasomo, kuwaleta wanafunzi pamoja lakini pia kuwaokoa wazazi kwenye gharama za ada za shule.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Elimu na Utamaduni Arusha, Sudha Majhitia alieleza umuhimu wa elimu katika kujenga mustakabali wa vijana katika ujenzi wa Taifa.
"Hii sio kwa ajili ya shule tu bali kwa ajili ya maisha yenu baadae, msingi huu ulioanza kujengwa sasa ni wa muhimu hasa kipindi hiki ambacho dunia inaenda kwa kasi ya teknolojia,"