Simulizi mzee mwenye upofu anavyotembea kilomita tisa kuuza mkaa

Mzee Abdu Hassan Mndonde mkazi wa Kitongoji cha Mtumbikile Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara mwenye ulemavu wa macho ajikata majani ya kusukia mkeka porini. Picha na Florence Sanawa.

Muktasari:

  • Mzee mwenye ulemavu wa macho kwa miaka 25 asimulia anavyotembea kilomita tisa akiwa na gunia la mkaa kichwani huku akitafuta wateja asema alipata ulemavu huo ukubwani.

Mtwara. Mkazi Ndumwe mkoani hapa Abdul Mndonde mwenye ulemavu wa macho, anayejishugulisha na biashara ya mkaa amesimulia namna anavyopambana ili kupata fedha za kujikimu kimaisha.

 Mdonde anasema kila siku anatembea zaidi ya kilomita tisa kwenda na kurudi kwa ajili ya kufanya biashara hizo zinazomsaidia kujikwamua kiuchumi. Mbali na hilo, Mndonde anajihushisha na usukaji wa mikeka.

Akizungumza na Mwananchi mzee huyo anayeishi Kitongoji cha Mtumbikile katika Halmashauri ya Hilaya ya Mtwara, amesema amezoea kufanya biashara bila kujali hali yake au changamoto anazokutana nazo kutokana na ulemavu wa macho.

Anasema kwa nyakati tofauti amekuwa akienda porini kukata majani maalumu ya kusukia mikeka anayoisuka na kuiuza.

Mndonde anasema anasema katika harakati hizo, muda mwingine anakuwa amebeba gunia la mkaa kichwani hali ambayo inawashangaza baadhi ya wananchi.


Alivyopata ulemavu wa macho

Mdonde amesema mwaka 1998 aliumwa na kupatwa na ulemavu wa macho yaliyomuanza kwa kumuuma na kumsababishia upofu uliodumu hadi sasa. Hata hivyo, anasema ameshazoea hali hiyo na anaendelea kutafuta ridhiki kama kawaida.

Mdonde anasema na watoto wawili waliozaliwa mwaka 1995 na 1996, akisema kati yao hao mmoja ni mlemavu wa kusikia.

“Licha ya watoto wangu kuwa na ulemavu lakini wao ndio walionipa mtaji wa biashara ninazofanya sasa. Wakat mwingine wao ndio wanaoendesha shuguli hizi nikiwa nimeenda porini au kuangaika.

“Hawa vijana mmoja akiwa hana tatizo, lakini mwingine alizaliwa akiwa na tatizo. Tunaishi kwa uwezo wa Mungu tunatembea tunapata chakula kidogo wakati mwingine hatupati kabisa, lakini tunaamini wapo Watanzania wanaoweza kutusaidia,” amesema.

 Kwa mujibu wa Mndonde, anatumia mimea ya Nduru inayotumika akutengeneza mikeka anayoiuza kwa Sh10,000, Sh8,000 na 6,000. Ametumia nafasi hiyo kuwaomba Watanzania watakaoguswa kumsaidia.

 “Natamani kumalizia nyumba yangu ambayo ni ya miti na udogo, nataka mimi na watoto wangu tulale katika mazingira salama zaidi. Lakini nashindwa kutokana na kipato tunachopata kinatosha katika matumizi ya kula,” amesema Mndonde.

Mkazi wa kitongoji hicho, Ally Makanjira anasema Mndonde anaishi katika mazingira magumu, lakini kutokana na uwezo duni wa majirani wenzake wanashindwa kumsaidia katika jitihada za kujenga, ingawa chakula wanampa.

“Maisha yake ni magumu, pia hali yake na kazi yake ni ngumu analima na kufanya shughuli mbalimbali ili kupata kipato cha kuendesha maisha yake. Haijalishi hali aliyonayo anapambana sana mzee huyu,” anasema Makanjira.