TCCIA wakaribisha wawekezaji Tanzania

Muktasari:

Rais  wa Chemba ya Wafanyabiashara wa Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) Paul Koyi amesema kufanya biashara kwa uadilifu,uwazi na kulipa kodi kwa wakati kutakuza maendeleo ya Tanzania na kuiwezesha Serikali kuwafikishia wananchi huduma muhimu.

Dar es Salaam. Rais  wa Chemba ya Wafanyabiashara wa Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) Paul Koyi amesema kufanya biashara kwa uadilifu,uwazi na kulipa kodi kwa wakati kutakuza maendeleo ya Tanzania na kuiwezesha Serikali kuwafikishia wananchi huduma muhimu.

 Kauli hiyo ameitoa jana Juni 10,2021 wakati akisaini makubaliano ya kufanya kazi na Jukwaa la wawekezaji kutoka Afrika Kusini wanaofanya shughuli zao hapa nchini(SABF).

Koyi amesema kwakuwa TCCIA inatengeneza mazingira wezeshi kwa wawekezaji kutoka nje lakini wana wajibu wa kufanya kazi nao na kubadilishana uzoefu ikiwemo kulipa kodi na kujenga baadhi ya huduma kwa jamii ya Tanzania.

“Mfano hapa mmesikia  Kampuni ya Geita Aglo Ashanti Maining ilikuwa inaongoza  kwa kulipa kodi kwa mwaka uliopita na wamekuwa wakitoa huduma muhimu ya  kujenga shule, kusaidia kilimo ni jambo zuri na inaonesha tunapokutana hivi tunabadilishana uzoefu,”amesema.

Naye Rais wa SABF  Manish Thakral amesema amefurahi kuingia kwenye ushirikiano na TCCIA  na watatumia fursa hiyo kuyakaribisha majukwaa mengine kwakuwa  mazingira ya uwekezaji hapa nchini ni mazuri.

Amesema kwa muda mrefu walikuwa  wanazungumza pamoja na TCCIA kuona  namna wanavyoweza kufanya biashara kwa ushirikiano.