Tembo wamtoa utumbo aliyetaka kupiga nao ‘selfie’

Muktasari:

  • Mkazi wa Kijiji cha Kiperesa wilayani Kiteto mkoani Manyara, Issa Shabni (32) amenusurika kifo na kulazwa hospitali ya Wilaya ya Kiteto baada ya kupigwa na tembo walioonekana wakirandaranda kijijini kwao.

Kiteto. Mkazi wa Kijiji cha Kiperesa wilayani Kiteto mkoani Manyara, Issa Shabni (32) amenusurika kifo na kulazwa hospitali ya Wilaya ya Kiteto baada ya kupigwa na tembo walioonekana wakirandaranda kijijini kwao.

Tembo hao wakionekana karibu na makazi yao wakila mahindi kisha watu kuwasogelea kutaka kupiga nao picha.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Manyara, RPC George Katabazi ameeleza kuwa Machi 12, 2023 tembo watatu walionekana Kijiji cha Kiperesa mchana wakiandaranda kwenye mashamba ya watu yaliyopo karibu na makazi yao.

Hao tembo hawakuwa na shida lakini waliaza kucharuka baada ya kundi lubwa la watu kuwasogelea na wengine kupiga picha, hali iliyowapa usumbufu kisha kumjeruhi mtu mmoja ambaye kwa sasa amelazwa hospitali ya Wilaya ya Kiteto.

"Ni kwamba majeruhi amelazwa hospitali ya wilaya ya Kiteto na anaendelea na matibabu,” amesema.

Jeshi la Polisi unatoa wito kwa wananchi kuacha kuwasogelea wanyama wakali kama tembo kwani kwa kufanya hivyo ni kuhatarisha maisha yao.

"Ni kweli tembo walifika Kijiji cha Kiperesa kata ya Olboloti na kumjeruhi mtu mmoja ambaye anaendelea na matibabu Hospitali ya Wilaya ya Kiteto, niwatake wananchi wachukue tahadhari ya wanyama hao," amesema RPC Katabazi.

Kaka wa majeruhi Shabani Kizuri akizungumzia tukio hilo, amesema baada ya kupata taarifa mdogo wake amejeruhiwa na na tembo ilikuwa kazi kwenda kumwokoa hapo kwa kuwa tembo hao walikuwa karibu na yeye haikuwa rahisi kusimama, alijeruhiwa zaidi.

"Hali ya mdogo wangu imeanza kuimarika baada ya kumfikisha hospitali ya Wilaya ya Kiteto na kupatiwa matibabu pamoja na kwamba tunatakiwa kumpeleka Hospitali ya Benjamin Mkapa Dodoma kwa matibau zaidi.

"Ndugu yangu alikanyagwa sana na tembo, alichomwa na pembe ubavuni utumbo ukatoka nje ila sasa hivi baada ya kupata matibabu hali yake siyo mbaya,  tunatafuta fedha tuende Hospitali ya Benjamin Mkapa kwa matibabu zaidi," alisema Kizuri.

Makamu wa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kiteto, Kassimu Msonde kutokana na sakata hilo, ameahidi kulifikisha kwenye vikao vya kisheria vya halmashauri ili lipatiwe ufumbuzi.

"Sasa hivi tembo ni wengi na wanazurura bila mpango, wananchi wachukue sasa tahadhari ili wasipate madhara zaidi,” amesema.