Usaili wa kuwasaka warembo wa Miss Grand Tanzania wiki ijayo

Muktasari:

  • Zoezi za usaili litakalosimamiwa na wadau wa urembo nchini litaanza saa 4.00 asubuhi na kufikia tamati saa 11.00 jioni.

Dar es Salaam.Usaili wa kuwatafuta washiriki wa mashindano ya kumtafuta mrembo wa Miss Grand Tanzania utafanyika Julai 10, mwaka huu katika ukumbi wa Dar es salaam Convention Centre, jijini Dar es Salaam.

Zoezi za usaili litakalosimamiwa na wadau wa urembo nchini litaanza saa 4.00 asubuhi na kufikia tamati saa 11.00 jioni.

Mratibu wa mashindano hayo nchini Abraham Mahimbo amewataka warembo wenye vigezo kuichangamkia fursa hiyo kwani ni mashindano yanayokuja kuleta mapinduzi katika fani ya urembo nchini.

Mahimbo amesema mashindano ya Miss Grand Tanzania ambayo yatakuwa chini ya Miss Grand International yanakuja kuleta mapinduzi na kuyapa heshima mashindano ya urembo nchini.

“Warembo wanaojiamini na waliotayari kwa mapinduzi ninawakaribisha katika usaili kwani nafasi hii ni adhimu ambayo hutokea mara moja tu katika maisha,” alisema Mahimbo.

Amevitaja vigezo vya kushiriki mashindano hayo ni umri wa kati ya miaka 18-27, urefu sentimita 168, ambaye hajaoelwa, hajawahi kupata mtoto,

ajue utamaduni na matukio yanayoendelea nchini, kisiasa, uchumi, mazingira, matatizo, awe na tabia njema na hajawahi kujihusisha na vitendo vya aibu kama biashara ya ngono.

Alisema siku ya usaili washiriki watatakiwa kuwasilisha vyeti vya kuzaliwa na fomu zinapatikana Swahili Studios- Magomeni, Merry Bright Beauty Point-Tabata, City Star Boutique- Namanga na Infinity Lounge Mbezi Beach.