UVCCM wamuonya Diallo, wadai anawadhihaki viongozi wastaafu

UVCCM wamuonya Diallo, wadai anawadhihaki viongozi wastaafu

Muktasari:

  • CCM imelaani kauli ya kubeza viongozi wastaafu iliyotolewa na mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Mwanza, Antony Diallo katika mahojiano aliyofanya na kituo kimoja cha televisheni nchini Tanzania.

Songwe. CCM imelaani kauli ya kubeza viongozi wastaafu iliyotolewa na mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Mwanza, Antony Diallo katika mahojiano aliyofanya na kituo kimoja cha televisheni nchini.

Kauli hiyo imetolewa leo Jumamosi Julai 10, 2021 na katibu mkuu wa umoja wa vijana wa chama hicho (UVCCM),  Kenani Kihongosi katika kikao cha majumuisho ya ziara ya kuimarisha chama inayofanywa na sekretarieti ya chama hicho ikiongozwa na katibu mkuu wa CCM,   Daniel Chongolo.

Kihongosi amesema kauli iliyotolewa na kiongozi huyo ni msimamo wake mwenyewe na si wa CCM na kwamba jumuiya ya vijana  inalaani kauli zinazotolewa na kiongozi huyo   kuwabeza  viongozi walioitumikia  nchi,  akitaka wastaafu hao kuachwa wapumzike.

"Tangu leo asubuhi tumeona ujumbe ukisambaa kwenye mitandao ya kijamii ikinukuu kauli iliyotolewa na mmoja na kiongozi ambaye anaingia kwenye vikao vya maamuzi lakini leo ameamua kutoa kauli hii ambayo imetuchukiza sana vijana kwani tulitegemea wawe wa kwanza kutuongoza, " amesema.

Kihongozi amesema kiongozi huyo wa CCM ambaye ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa  amenukuliwa akisema viongozi wengine wanaoteuliwa na CCM wanapaswa kuwa hospitali ya magonjwa ya akili ya Mirembe iliyopo mkoani Dodoma.