VAT yarejeshwa bidhaa za Tanzania Bara, Zanzibar

Muktasari:

  • Serikali inapendekeza kufanya marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ili kurudisha utaratibu wa kurejesha VAT kwa bidhaa zinazonunuliwa Tanzania Bara na kutumika  Zanzibar.

Dar es Salaam. Serikali inapendekeza kufanya marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ili kurudisha utaratibu wa kurejesha VAT kwa bidhaa zinazonunuliwa Tanzania Bara na kutumika  Zanzibar.

Pia serikali  inapendekezwa marejesho ya VAT yatakayofanyika kwa bidhaa zinazotoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar yafanyike pia kwa bidhaa zitakazotoka Zanzibar kwenda Tanzania Bara sambamba na marekebisho ya vifungu husika vya sheria za VAT kwa pande zote mbili za muungano.

Kutokana na utaratibu huu, kiwango cha asilimia sifuri ya VAT  kilichokuwa kinatozwa bidhaa hizo kitasitishwa.

Hayo yameelezwa leo Alhamisi Kuni 10, 2021 bungeni mjini Dodoma na Waziri wa Fedha na Mipango Dk Mwigulu Nchemba wakati akiwasilisha bajeti kuu ya Serikali mwaka 2021/22 .

Amesema hatua hiyo  inatokana na mfumo wa kutoza VAT kwa kiwango cha asilimia sifuri kwa bidhaa za viwandani pekee kutowanufaisha wafanyabiashara wa Zanzibar wanaonunua bidhaa na kodi ya ongezeko la thamani Tanzania Bara na kutozwa tena kodi hiyo pindi bidhaa hizo zinapopelekwa visiwani humo.

Dk Mwigulu ameeleza hatua hiyo inalenga  kuwa na ufanisi wa marejesho, maboresho ya mifumo.