Vijana washauriwa kutumia mitandao kujikwamua kiuchumi

Muktasari:

  • Vijana nchini wameshauriwa kuacha tabia ya kutumia vibaya mitandao ya kijamii na mifumo ya kidijitali badala yake wamehimizwa kuitumia kutafuta fursa mbalimbali za mafunzo na biashara ili kujikwamua kiuchumi.

Dar-es-Salaam. Vijana nchini wameshauriwa kuacha tabia ya kutumia vibaya mitandao ya kijamii na mifumo ya kidijitali badala yake wamehimizwa kuitumia kutafuta fursa mbalimbali za mafunzo na biashara ili kujikwamua kiuchumi.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Shirika lisilo la Kiserikali linalojishughulisha na utoaji wa elimu ya matumizi sahihi ya kidijitali (DA4TI), Peter Mmbando wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo vijana katika masuala ya usalama wa kidigitali.

Mmbando amesema katika karne ya sasa ipo haja vijana kuchangamkia fursa mbalimbali zilizopo katika mitandao ya kijamii kuliko kuitumia vibaya.

“Tunachotaka kufanya sisi ni kuwaelimisha vijana kufanya matumizi yenye tija katika mitandao, leo tupo hapa kuwaeleza vijana kuwa wanaweza kupata kazi kwa kuandika makala mbalimbali na kutengeneza video nzuri zinazohusiana na mazingira na kupinga unyanyasaji na kisha kuweka katika mtandao,” amesema

Hata hivyo amefafanua kuwa biashara za kimtandao zinakosa uaminifu kwa kiasi kikubwa kutokana na baadhi ya watu kuitumia kutapeli watu kwa kutangaza biashara bandia na kuwaibia.

Ameongeza kuwa ili kupunguza utapeli katika mitandao shirika lao limeamua kutoa elimu kwa kundi hilo la vijana juu ya namna ya kuepukana na wizi mtandaoni.

“Tumeanza na vijana hawa tutaendelea kwenda shule mbalimbali na kuwaeleza kwamba wanaweza kutumia mtandao kwa kusoma, kutafuta kazi na kuelimisha jamii hasa kuwa na maadili, pia wanatakiwa kujua siyo kila kitu wanaweza kuweka mitandaoni bali unapaswa kuchuja na kujiridhisha kabla ya kuweka habari mitandaoni,” amesema

Kwa upande wa Hiari Kikule ambaye ni mmoja wa wanufaika na mafunzo hayo, amesema kuwa mitandao ina umuhimu mkubwa ingawa ina haribiwa na watu wachache wasiojua umuhimu wake.

Kikule ambaye ni Mtetezi wa haki za binadamu kwa njia ya mtandao, amesema katika mafunzo hayo wamejifunza namna ya kujilinda na matapeli wa mtandaoni  na jinsi ya kuhakikisha vyombo vyao wanavyovitumia kusambaza taarifa vinakuwa salama.

Naye Mhitimu Chuo Kikuu cha Dodoma (UDSM) katika Shahada ya Habari na Taarifa mitandaoni, Irene Dafrine amesema  katika mafunzo hayo amejifunza namna ya kufanya kuhakikisha taarifa anazozichapisha mitandaoni zinakuwa salama.

“Kwanza natakiwa kuwa na uhakika wa taarifa ninayotaka kuweka mitandaoni ili nikija kuulizwa niwe na majibu ya kutosha ili kuzuia taarifa kuleta taharuki katika jamii,” amesema