Wakurugenzi watano MSD waenguliwa

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya feda ya Wizara hiyo kwa mwaka ujao wa fedha.

Muktasari:

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema Wizara hiyo imewaondoa kwenye nafasi zao wakurugenzi watano wa Bohari ya Dawa Tanzania (MSD) kutokana na malalamiko yaliyokuwa yakitolewa.

Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema Wizara hiyo imewaondoa kwenye nafasi zao wakurugenzi watano wa Bohari ya Dawa Tanzania (MSD) kutokana na malalamiko yaliyokuwa yakitolewa.

Waziri Ummy amesema hayo jana Jumatatu Mei 16, 2022 jijini Dodoma wakati akihitimisha mjadala wa bajeti kwa wizara hiyo kwa mwaka wa fedha wa 2022/2023, baada ya kuchangiwa na wabunge mbalimbali.

Amesema kuwa “Pamoja na Rais Samia Suluhu Hassan kubadilisha uongozi wa juu wa MSD na kumteua mwenyekiti mpya wa bodi, hatua hiyo ilikuwa haitoshi kutokana na malalamiko mengi yaliyokuwa yakitolewa.

Waziri Ummy ametaja wakurugenzi wanaoondolewa kuwa ni pamoja na “Mkurugenzi wa Fedha anaondoka MSD, Mkurugenzi wa manunuzi MSD, Mkurugenzi wa Logistics MSD, Mkurugenzi wa Sheria MSD na Mkurugenzi wa Utawala wa MSD anaondoka.” amesema Waziri Ummy

Mei 9 mwaka huu Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwa kwenye ofisi za MSD aliiagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuwashughulikia watumishi wote watakaoonekana wamehusika katika ubadhirifu wa manunuzi na fedha katika Bohari ya Dawa (MSD).

Takukuru ambao walikuwa tayari wameweka kambi katika taasisi hiyo, walikuwa wanafanya ukaguzi katika yale yaliyoonekana katika ripoti ya ukaguzi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere pamoja na maeneo mengine ikiwemo fedha za Uviko-19.