Wanandoa wapya waliofariki ajalini wazikwa Chunya

Majeneza yenye miili ya wanandoa Noah Semfukwe (30) na Agnes Kiyeyeu (27) waliofariki dunia Jumanne Desemba 13, 2022 kwa ajali ya gari eneo la Tanangozi, nje kidogo ya Manispaa ya Iringa ambayo imezikwa leo katika kijiji cha Makongolosi, Chunya mkoani Mbeya.

Muktasari:

  • Wanandoa hao, Noah Semfukwe (30) na Agnes Kiyeyeu (27) waliofariki dunia Jumanne Desemba 20, 2022 kwa ajali ya gari eneo la Tanangozi, nje kidogo ya Manispaa ya Iringa wamezikwa leo katika kijiji cha Makongolosi, Chunya mkoani Mbeya.

Chunya. Miili ya wanandoa wapya ambao ni askari polisi Mkoa wa Arusha waliofariki dunia kwa ajali ya gari eneo la Tanangozi, nje kidogo ya Manispaa ya Iringa imezikwa leo Ijumaa Desemba 23, 2022.

Wanandoa hao, Noah Semfukwe (30) na Agnes Kiyeyeu (27) walifariki dunia Jumanne wiki hii wamezikwa katika kijiji cha Makongolosi, Chunya mkoani Mbeya.

Noah na Agness waliodumu kwenye ndoa kwa siku tatu, ambapo walifunga pingu za maisha Desemba 17 mwaka huu, walifariki dunia kwenye ajali ilitokea katika eneo hilo wakati gari dogo aina ya Vits iliyokuwa ikiendeshwa na Noah ilipopanda tuta na mbele yake kukawa na lori, hivyo wakati analikwepa akakutana uso kwa uso na basi la Luwizo lililokuwa likitokea Njombe kwenda Dar es Salaam.

Katika ajali hiyo watu watatu walipoteza maisha, akiwemo Enocka Mbata (35), mkazi wa Iringa aliyekuwa kwenye gari hilo na mwili wake ulizikwa juzi Iringa.

Leo, miili hiyo imezikwa katika Halmshauri ya Wilaya ya Chunya mkoani Mbeya huku ndugu wa upande wa mwanaume wameeleza kuwa marehemu alikuwa tegemezi kwenye familia kufariki kwake amewaachia pengo ambalo haliwezi kuzibika.

Kaka yake Noah, Mathias Simfukwe ameeleza kuwa siku aliyofariki mdogo wake huyo alikuwa anakuja Chunya kwaajili ya msiba wa mtoto wa kaka yao.

Baadhi ya polisi wakiwa wamebeba jeneza lenye mwili wa mmoja ya wanandoa waliofariki dunia Jumanne Desemba 13, 2022 kwa ajali ya gari eneo la Tanangozi, nje kidogo ya Manispaa ya Iringa wamezikwa leo katika kijiji cha Makongolosi, Chunya mkoani Mbeya.

"Mdogo wangu alikuwa mtu wa kujitoa sana kwenye familia yetu hivyo baada ya kupata taarifa hizo tulistushwa sana na msiba kwani tulitupata tukiwa kwenye msiba wa mtoto wa kaka yetu.

Braytness Mwanjabe ambaye ni wasimamizi wa ndoa ya hao marehemu hao amesema alipigiwa simu na rafiki yake akimtaarifu kuhusu kifo cha wanandoa hao.

"Nimekuwa nikifahamiana na marehemu hao kabla ya hawana hata mtoto mmoja tulikuwa tunaishi kama ndugu mpaka wanabahatika kupata watoto hadi kufikia kufunga ndoa nimeumizwa sana na msiba huu;

Nilikuwa nimetoka kuwasiliana na Agnes muda mfupi kabla ya kifo chake tukizungumzia siku ya ndoa ya na mambo mengine yaliyokuwa yakihusu siku ya ndoa” amesema msimamizi huyo wa ndoa ya wawili hao.