Wataalamu wa fedha nchini waaswa kuwa waadilifu

Naibu mkuu wa chuo taaluma utafiti na ushauri wa kitaalamu Chuo cha Uhasibu Arusha, Profesa Epaphra  Manamba akizungumza chuoni hapo.

Muktasari:

Wataalamu wa Fedha na Mahesabu nchini wameaswa kuwa waadilifu wanapotekeleza majukumu yao na kuwa washauri wazuri kwa jamii katika kufafanua dira ya maendeleo ya uchumi nchini.

Arusha. Wataalamu wa Fedha na Mahesabu nchini wameaswa kuwa waadilifu wanapotekeleza majukumu yao na kuwa washauri wazuri kwa jamii katika kufafanua dira ya maendeleo ya uchumi nchini.

Hayo yamesemwa  leo Novemba 12  jijini  Arusha  na Kamishna msaidizi idara ya uendelezaji wa sekta ya fedha wizara ya Fedha na Mipango, Janeth  Hiza wakati akizungumza katika siku ya wahasibu duniani iliyofanyika  katika chuo cha uhasibu Arusha .


Hiza amesema kuwa,wataalamu hao wanapaswa  kuwa waadilifu na kutanguliza weledi katika utendaji kazi wao kwani idara hiyo  ni muhimu  sana kwa malachi ya nchi kwa ujumla. 

Aidha amewataka wahasibu kuhakikisha wanajifunza udhibiti  wa fedha haramu,pamoja na kuhakikisha wanajiunga na bima mbalimbali kwa ajili ya maendeleo  yao .

"Nawaombeni sana mkajifunze kupata huduma jumuishi za fedha na mkatumie elimu zenu kufundisha jamii kuhusu elimu juu ya matumizi ya fedha na nidhamu ya fedha kwa ujumla kwani nyie ndio mnaotegemea katika jamii nzima inayowazunguka."amesema.


Kwa upande wake Naibu Mkuu wa chuo taaluma utafiti na ushauri wa kitaalamu Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), Profesa Epaphra Manamba  amewataka wahasibu  hao kuhakikisha wanafanya kazi kulingana na sheria na taratibu zilizopo  huku  wakifuata maadili na matumizi  sahihi ya fedha. 


Profesa  Manamba amewataka wanafunzi kufanya kazi kulingana na elimu na maadili  waliyopata  chuoni hapo  ili wakawe  mfano wa kuigwa katika jamii. 


Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa idara ya fedha na uhasibu  wa IAA, Dennis Hyera  amesema kuwa siku ya wahasibu duniani kwa mara  ya kwanza iliadhimishwa mwaka 1972 na wanajumuiya  ya CPA wa San Diego Chapter katika taasisi ya Management  Accountants .


Hyera amesema kuwa, siku  ya wahasibu  duniani imeanzishwa kwa ajili ya kuwahamasisha  vijana walioko kwenye tasnia nzima ya uhasibu  mnamo mwaka 1976 taasisi  mbalimbali  zilialikwa rasmi kusherehekea  siku ya wahasibu duniani na ikarasimishwa kusherehekewa mahali popote na nchi yoyote kila ifikapo Novemba 10 kila mwaka .

Makamu wa Rais Serikali ya Wanafunzi (IAASO), Shazma Edward amesema kuwa kupitia siku ya wahasibu duniani wamejifunza mambo mengi ikiwemo  kutanguliza maadili na uzalendo katika utendaji  kazi wao wa  kila  siku ili taaluma hiyo  iendelee kuboreka  zaidi.