Watoto watatu wadaiwa kumuua mama yao

Muktasari:

  • Watoto watatu wa familia moja wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani hapa kwa tuhuma za kumuua mama yao mzazi kwa kumkatakata na kitu chenye ncha kali kichwani na mkononi.

  

Geita. Watoto watatu wa familia moja wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani hapa kwa tuhuma za kumuua mama yao mzazi kwa kumkatakata na kitu chenye ncha kali kichwani na mkononi.

Watoto waodaiwa kumuua mama yao ni Jumbe Kifoda (36), Doto (34) na Rukina Kifoda (30).

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Henry Mwaibambe leo Juni 2, 2022 amethibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Amedai kuwa mauaji hayo yametokea usiku wa  kuamikia Juni mosi, 2022 katika Kijiji cha Nyaruyeye, Kata ya Busanda wilayani Geita.

Kamanda amedai kuwa chanjo cha mauaji hayo ni watoto kudai shamba la urithi na mama kusema hawezi kutoa kwa kuwa ameshawalea na kuwataka waondoke nyumbani wakajitegemee.

Mwili wa marehemu umezikwa jana nyumbani kwake baada ya kufanyiwa uchunguzi.

Watuhumiwa watafikishwa kwenye vyombo vya sheria wakati wowote kuanzia sasa kujibu mashtaka yanayowakabili.

“Inadaiwa mama yaoaliwataka waondoke nyumbani kwake na alishawafukuza lakini wakawa wanarudi kudai mashamba ya urithi akawa anakataa wakawa wanamtishia kuwa watakuja kumuua kama hatawapa mashamba tunaamini hawa ndio wamemuua mama yao kwa kuwa mara nyingi watu wa kanda hii wakisema wataua ujue wataua kweli”

Mwaibambe amesema jeshi hilo limeandaa kikosi kazi cha kupambana na wauaji kwa kuwa mauji kama hayo yalikuwa yakitokea miaka ya nyuma na kudaiwa ni Imani za kishirikina lakini ukweli ni kuwa yanayochangia mauji kanda hii ni mengi ikiwemo mausuala ya urithi.

Kamanda amewataka vijana kujishughulisha na kutafuta mali zao wenyewe badala ya kuwa tegemezi kwa kutegemea urithi wa wazazi