Waumini watakiwa kusamehe
Waumini katika Kanisa la TAG City Christian Center (CCC) Upanga wakifurahia katika mkesha wa Krismas jijini Dar es Salaam. Picha na Victor Tullo
Muktasari:
- Waumini katika kanisa la TAG City Christian Center (CCC) Upanga jijini Dar es Salaam wametakiwa kuwa na moyo wa kusamehe wakiwemo watoa huduma.
Dar es Salaam. Waumini katika Kanisa la TAG City Christian Center (CCC) Upanga jijini hapa, wametakiwa kuwasamehe ndugu, rafiki na watoa huduma.
Akizungumza katika Mkesha wa kuikaribisha sikukuu ya Krismasi kanisani hapo Mchungaji msaidizi Dk Charles Sokile amesema amani ni jambo la muhimu na ili kuwa nayo waumini hawana budi kusameheana.
“Kuna watu hawana amani na Kila mtu, hawana amani na Serikali, hawana amani na vyama vya siasa, hawana amani na watoza ushuru. Katika majira haya tafuta kuwa na amani na kila mtu," amesema Mchungaji Dk Sokile.
Mchungaji Dk Sokile amesema ili watu wamuone Mungu ni muhimu kuwa na amani na kila mtu katika jamii kwani, kuzaliwa kwa Yesu Kristo ni ishara ya amani ulimwenguni.
"Kama Kuna mtu amekukosea tafadhali msamehe. Anapokuomba msamaha mpigie simu muambia mimekusamehe, na hivyo ndivyo anavyotaka Mungu," amesema.
Amewataka waumini kutumia fursa ya amani nchini kuyaombea mataifa yanayopitia katika nyakati za vita akiyataja; Ukraine, Russia, Israel na Palestina.
Wakristo duniani leo Desemba 25, 2023 wanaadhimisha sikukuu ya Krismasi ikiwa ni kumbukumbu ya kuzaliwa kwa mkombozi wao Yesu Kristo.