Wingi wa kemikali inayoingizwa nchini wailemea ofisi ya mkemia mkuu

Mkemia Mkuu wa Serikali, Samwel Manyele

Muktasari:

  • Akizungumza leo Alhamisi, Agosti 17 jijini Dar es Salaam, Mkemia Mkuu wa Serikali, Samwel Manyele amesema ongezeko hilo linatokana na waagizaji wengi kuagiza mzigo wa kemikali bila kufuata sheria.

Dar es Salaam. Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali imesema imelemewa na kiwango kikubwa cha kemikali za matumizi ya nyumbani na viwandani zinazoingizwa nchini kwa siku.

Akizungumza leo Alhamisi, Agosti 17 jijini Dar es Salaam, Mkemia Mkuu wa Serikali, Samwel Manyele amesema ongezeko hilo linatokana na waagizaji wengi kuagiza mzigo wa kemikali bila kufuata sheria.

Amesema kabla ya mwaka 2013 walikuwa wakitoa vibali vitano hadi saba kwa siku, lakini kuanzia mwaka huo wamekua wanatoa vibali 100 hadi 150 kwa siku huku wakilazimika kufanya kazi saa 24.

"Sheria inamtaka muagizaji wa kemikali kuomba kibali, kusajiliwa kabla ya kuagiza mzigo, lakini walio wengi wanakiuka sheria kwa kuagiza mzigo ukiwa bandarini ndiyo wanaanza kuomba nyaraka hizo muhimu," amesema Profesa Manyele.

Profesa Manyele amesema mrundikano wa mizigo unakuwa mkubwa kutokana na kuwa na wafanyakazi wasiofika 100 nchi nzima.

"Kuna vituo vingi vya kupokelea kemikali, ndani ya bandari vipo sita na nje vipo 17.

" Kutokana na wingi huo wakaguzi wanalazimika kutumia muda mwingi kutembea kufuata mizigo ilipo,"amesema Profesa Manyele.