Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Dk Kijo Bisimba: Wazazi wa miaka hii wanachoka sana

Dar es Salaam. “Ni kweli harakati za kutafuta maisha zinachosha, lakini sikubaliani na namna wazazi wa miaka hii wanavyochoka kiasi kwamba wanakosa muda wa familia. Watoto wanaachwa chini ya uangalizi wa watu wengine ambao huenda hawana wajualo kuhusu malezi.

“Unakuta wazazi wako Dar es Salaam wanachukua msichana wa kazi kutoka mkoani, hawamfahamu wala kujua malezi yake huko alikotoka, unamuachia watoto wako ndiye akulelee unategemea nini kitatokea, halafu tunalalamika mmomonyoko wa maadili, tunakuwaje na maadili wakati hatutaki kulea watoto wetu.”

Hayo ni maneno ya Mkurugenzi mstaafu wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) na mwanaharakati mkongwe, Dk Hellen Kijo Bisimba wakati wa mahojiano aliyofanya na jarida la Familia.

Dk Hellen, ambaye ni mama wa watoto wanne na wajukuu 11 anasema kwa mwenendo wa wazazi kukosa muda wa kuwa na watoto wao, suala la mmomonyoko wa maadili litaendelea kuwa tatizo kubwa kwa sababu misingi ya malezi haizingatiwi.

Mama huyu anasema kinachoendelea sasa ni tofauti na ilivyokuwa awali, kwa sababu licha ya wazazi kuwa wafanyakazi, walikuwa wanatenga muda wa watoto.

Akijitolea mfano yeye wakati anafanya kazi, anasema alikuwa anaweka ratiba zake vizuri ili apate muda wa familia na kama mama alikuwa akiingia huku na kule kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri nyumbani kwake.

“Kiukweli, huwa nashangaa hivi kwa nini vijana wa siku hizi wanachoka namna hii, yaani mama anarudi nyumbani kutoka kwenye mihangaiko yake anakwambia amechoka kiasi kwamba anapita na kwenda kujifungia chumbani au kukaa na simu yake.

“Hali iko hivyo hivyo kwa baba, hata kama atatoka mapema kwenye shughuli zake atapita sehemu za starehe au kwenye vijiwe akae na wenzie, atarudi nyumbani usiku akiwa amechoka, majukumu yote ya mtoto anaachiwa dada, haya mambo hayakuwepo zamani,” anasema mama huyo.

Anasema licha ya wazazi wengi kusingizia wanabanwa na majukumu ya kutafuta kipato, teknolojia pia inachangia kupoteza muda mwingi wa familia kuwa pamoja.

Dk Hellen anasema: “Siku hizi mama yupo kwenye simu, baba anaangalia mpira au baa na wenzie, hawapati muda wa kukaa na watoto na kuwajenga katika misingi bora, halafu tunalalamika hakuna maadili. Yaani mzazi unaishi na mwanao na hufahamu changamoto zake wala mambo anayopitia.

“Niwakumbushe kwamba maadili sio kitu kinachotokea hewani, kinatengenezwa kuanzia chini kwenye ngazi ya familia hadi jamii, sasa kama kuna mahali hapajakaa vizuri ndiyo tunakutana na haya ya mmomonyoko wa maadili, unasikia mtu amebaka watoto,” anasema Dk Hellen.

Akilinganisha hali ilivyokuwa miaka ya zamani, anasema suala la malezi lilihusisha jamii nzima na haikuwa ajabu mtu kumuwajibisha mtoto wa asiye wake.

Lakini hivi sasa hali imebadilika, hakuna anayethubutu kujihusisha na mtoto wa mwenzake.

“Zamani mtoto alikuwa wa jamii, ilikuwa mzazi ukimkuta mtoto anafanya vitu vya ajabu hata kama siyo wake, alikuwa anamuadhibu, lakini siku hizi kila mtu na mtoto wake na ukijaribu kujihusisha na mtoto asiyekuhusu jiandae kufungiwa kibwebwe, sasa haya siyo maisha. Hatupaswi kulea watoto kwa mwenendo huu, lazima turudishe mfumo wa malezi ya jamii,” amesema.


Maisha ya kustaafu

Baada ya kufanya kazi kwa miaka 41 katika kada mbalimbali, ikiwemo ualimu, sheria na asasi za kiraia hatimaye mwaka 2018 Dk Hellen alihitimisha safari yake ya utumishi wa umma na kustaafu rasmi.

Miongoni mwa vitu ambavyo anakiri hakujiandaa navyo ni maisha baada ya kustaafu, kutokana na hilo, Dk Hellen anawasisitiza vijana walioko kazini kujiandaa kwa ajili ya maisha yao ya baadaye.

Anasema katika miaka yote aliyofanya kazi hakuwahi kufikiria kuandaa maisha yake baada ya kustaafu, jambo lililomfanya hata asiwe na mpangilio mzuri wa matumizi ya fedha alizozipata baada ya kuhitimisha maisha yake ya ajira.

“Kiukweli sikuwa nimeandaa maisha baada ya kustaafu, kosa ambalo sitaki vijana waliopo kazini kwa sasa wafanye, naona huko serikalini huwa wanapewa semina za mwezi mmoja kabla ya kustaafu, kiukweli hiyo haisaidii, mtu anatakiwa kuanza kujiandaa kuishi maisha ya ustaafu mapema akiwa kazini.

“Binafsi sikuwa na elimu ya uwekezaji, akili na nguvu yangu yote ilikuwa kwenye kazi, hivyo hata ilipotokea nimestaafu nikapewa pesa zangu niliona siwezi kuanzisha kitu ambacho sina uzoefu nacho, hivyo nilitumia zile pesa kidogokidogo hadi zikaisha,” anasema Dk Hellen na kuongeza;

“Niliwahi kupata fedha nyingi za mafao wakati huo nilikuwa naenda kufanya PhD Uingereza, mtoto wangu wa mwisho alikuwa amemaliza kidato cha sita, nikaona niende naye akasome digrii ya kwanza, kwa hiyo fedha zangu nikazitumia kumsomesha. Niliporudi nikaendelea na kazi na nikapata hela, lakini sikuwa nafahamu hayo mambo ya hati fungani, huenda ningekuwa vizuri kiuchumi lakini sikuyajua,” anasema.

Anasema kutokana na kutokuwa na elimu ya uwekezaji, alipopata mafao yake ya hifadhi ya jamii na fedha alizoingiziwa na shirika lake kutokana na utumishi wake uliotukuka, alizitumia bila mpangili mzuri.

“Kwa kawaida sina tabia ya kumnyima mtu kitu kama ninacho, sasa nilipopata zile hela za kustaafu za mwisho mtu akija mama nina shida hii nampa, mara mama nina harusi ya mdogo wangu nampa, kwa kifupi nilitumia zile fedha hadi zikaisha nimebani sina hela.

“Uzuri ni kwamba naishi na mtoto wangu ambaye ananihudumia na kuhakikisha ninapata mahitaji madogo madogo, ikiwemo hela za sadaka na gari yangu inakuwa na mafuta ya kunipeleka kanisani na kunirudisha, nimemwambia wala asihangaike kunipa fedha nyingi maana nitazitumia tu,” anasema.

Anasema haikuwa rahisi kwake kuanza maisha mapya baada ya kufanya kazi kwa miaka 41 na kujihusisha na mambo mengine mengi yaliyokuwa yakimfanya asitulie sehemu moja kwa muda mrefu, hali iliyompa wakati mgumu katika siku zake za awali za kustaafu.

“Katika siku za awali nilipata tabu, haikuwa rahisi kukubaliana na ukweli kwamba muda wangu wa kufanya kazi umekwisha hivyo natakiwa kupumzika. Nikawaza na kufikia uamuzi kwamba siwezi kulima wala kuwa mfugaji lakini naweza kuendelea kuitumia akili yangu kufanya kazi.

“Nikatengeneza ofisi nyumbani kwangu, nikawa naendelea kuamka asubuhi najiandaa naingia ofisini kwangu ambako nimekuwa nikifanya shughuli mbalimbali, ikiwemo uandishi wa kitabu ambacho kimebeba historia ya maisha yangu na kazi zangu,” anasema.

Mbali na uandishi wa kitabu na kazi nyingine zinazohusisha taaluma ya sheria, Dk Hellen anasema anautumia muda wa kustaafu kuwa karibu zaidi na familia yake, shughuli za kanisani na kusoma vitabu.