Tehama inavyoweza kutumika katika kufundishaji, kujifunza

Kompyuta ni moja ya nyenzo nzuri za Tehama inayoweza kusaidia mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji. Picha ya Maktaba

Muktasari:

Walimu na wanafunzi wanatumia vifaa vya Tehama kama simu na kompyuta kwa mambo yasiyokuwa ya kimasomo

Kuanzia mwaka 2011 hadi 2013, nilikuwa mmoja wa wawezeshaji wa mradi wa kuwawezesha walimu wa shule za sekondari kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) katika mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji.

Mradi huu ujulikanao kwa jina la Science, Maths and English -ICT Project, ulikuwa unatekelewa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Mradi ulilenga masomo ya sayansi, hesabu na lugha ya Kiingereza. Kwa mujibu wa tafiti, masomo haya yalionekana kuwasumbua wanafunzi, hivyo mradi ulikuwa ni mpango wa majaribio wa kutafuta namna bora ya kukabiliana na changamoto hii shuleni.

Walimu walifundishwa namna ambavyo wangeweza kutumia kompyuta pamoja na vifaa vingine kama projekta kwenye ufundishaji.

Lengo kuu lilikuwa ni kutumia Tehama katika kurahisisha ufundishaji wa dhana ngumu ambazo hata pamoja na ufafanuzi wa mwalimu, bado zisingeweza kueleweka kwa wanafunzi.

Kwa mfano, katika somo la Biolojia, mada kama za mifumo ya mmeng’enyo wa chakula, damu na utoaji taka, mwalimu anaweza kutumia vifaa vya Tehama kutazama video au picha zinazoonyesha ufanyaji kazi wa mifumo hiyo.

Zana za Tehama

Katika makala haya, nalenga kumuelekeza mwalimu namna anavyoweza kupata zana za kidijitali za kufundishia na kujifunzia na anavyoweza kuzitumia.

Zana za kidijitali za kufundishia na kujifunzia zinaweza kuwa ni video, tovuti, picha mnato na za kucheza, sauti. Lakini pia unaweza kutumia maandishi yaliyomo kwenye vitabu au kwenye majarida.

Kwa wanaopendelea picha za kucheza, lazima wawe na kompyuta zenye vitumizi kama vile Java na adobe flash player. Vitumizi hivi vinaweza pia kupakuliwa mitandaoni.

Moja ya tovuti nzuri zenye mkusanyiko wa zana za kidijitali za kufundishia na kujifunzia ni PHET. Hadi sasa, tovuti hii ina zaidi ya maelezo milioni 200 ya masomo ya Kemia, Fizikia, Biolojia, Hisabati na mengineyo.

Zana hizi zilizomo kwenye tovuti hii ni za bure. Mwalimu, mwanafunzi au mwingine yeyote hana haja ya kuzinunua, ila unaweza kuchangia kama sehemu ya kuwezesha timu ya waandaaji kufanya kazi yao kwa uzuri zaidi.

Habari njema pia ni kuwa, maelezo haya katika tovuti ya PHET huweza kupakuliwa kirahisi na kuweza kutumiwa bila hata ya kuwa na intaneti. Jambo la kufanya ni kupakua “installer” yake na kisha kuziweka kwenye kompyuta yako.

Tovuti nyingine nzuri ni Absorblearning.com. Tovuti hii ina mkusanyiko wa video, maelezo, na picha katika masomo ya Kemia, Fizikia, Hisabati, na elimu ya elektroniki.

Hata hivyo, zana za kidijitali katika tovuti hii zinahitaji kulipiwa ili uweze kupakua na kutumia bila intaneti.

Uzuri wake ni kuwa, inawezekana kutumia zana hizi ukiwa umeunganishwa na intaneti.

Ukitaka kutumia tovuti hii, chagua somo unalohitaji kwa kuingia kwenye absorb Chemistry, absorb Physics, absorb Mathematics, absorb advanced physics au absorb Electronics na kisha nenda kwenye kiunganishi kinachoonyesha idadi ya zana zilizopo kwenye somo husika. Kisha tafuta zana kulingana na kile unachokisoma.

Mtandao wa YouTube pia una video nyingi na nzuri kwa ajili ya walimu na wanafunzi. Tutorvista ni moja ya watumiaji wa YouTube wanaopakia video za kielimu za masomo ya sayansi kwa shule za sekondari.

Unaweza kuzipakua video hizo na kuzitumia wakati wowote bila ya kunganishwa kwenye intaneti.

Ili kukwepa gharama zaidi za intaneti, ni vyema mwalimu au mwanafunzi akapakua video anazoona zinafaa kuliko kuziangalizia mtandaoni.

Moja ya kitumizi kizuri cha kupakulia video ni ‘internet download Manager’ (IDM). Kama ni mara yako ya kwanza kuitumia kwenye kompyuta yako, utaweza kuitumia kwa siku 30 na kisha utatakiwa kuinunua.

Baadhi ya tovuti nyingine ambazo unaweza kupata zana za kidijitali za kufundishia na kujifunzia ni pamoja na Math open reference iliyo na mkusanyiko wa maelezo ya mada ya jiometri kwa shule za sekondari na learnerstv, yenye mkusanyiko wa zana za masomo mbalimbali.

Kompyuta kama zana

Pamoja na kuwa kwa sasa, walimu wengi wanamiliki kompyuta, changamoto iliyopo ni kuwa, wengi hawana mazoea ya kutumia kompyuta na mtandao wa intaneti katika ufundishaji.

Nakumbuka katika shule fulani, ilikuwa vigumu kuwashawishi walimu kuandaa notisi, maandalio na maazimio ya kazi kwa kutumia kompyuta.

Hali kadhalika wanafunzi wengi wanatumia kompyuta na simu kwa mambo yasiyo ya kimasomo.

Mwandishi ni mtaalamu wa mifumo ya kompyuta. 0786806028