Muna Love adai corona imefanya waitwe matapeli

Ugonjwa wa Corona umeathiri maisha ya watu mbalimbali wakiwemo wajasiriamali wanaokwenda kuchukua bidhaa nje ya nchi.

Mmoja wa walioathirika na kuwepo kwa ugonjwa huo ambao tayari Shirika la Afya Duniani (WHO) limetangaza kama janga la Dunia ni msanii wa filamu na mjasiriamali Muna Love.

Muna Love ambaye jina lake halisi ni Rose Alphonce kwa muda sasa amekuwa akifanya biashara ya kwenda kuchukua nguo nchini China.

Hata hivyo alisema kutokana na ugonjwa wa corona, biashara hiyo imesimama kwa sasa na mbaya zaidi tayari alikuwa ameshachukua fedha kwa baadhi ya wateja.

“Wateja wengine wamekuwa hawaelewi hata unapowaeleza kuhusu janga la uwepo wa corona na kujikuta wakitupa majina mbalimbali ikiwemo kutuita matapeli.

“Japokuwa wapo baadhi wamekuwa waelewa kwa kuwa ndio janga linalozungumziwa sasa hivi duniani. Kikubwa nawaomba tuvumiliane katika hali hii kwani hata sisi tulishatanguliza fedha kwa tuliokuwa tunafanya nao biashara na hata ukisema urudishe huwezi kumridhisha kila mtu.

“Pia elimu iendelee kutolewa mara kwa mara ikiwemo kwa sisi wasanii bila kujali tutalipwa nini kwa kuwa ugonjwa huu unaweza kumkuta mtu yoyote,” alisema Muna.