Polisi Kigoma yazuia mkutano wa Zitto Kabwe

Muktasari:

Polisi Kigoma yazuia mkutano wa Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe kutokana na sababu za kiusalama, wenyewe wasema sababu hizo hazina mashiko bali zinalenga kumzuia mbunge huyo asitekeleze majukumu yake.

Dar es Salaam. Polisi mkoani Kigoma nchini Tanzania limezuia mkutano wa hadhara wa Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe uliopangwa kufanyika leo Ijumaa Januari 17,2020.

Kwa mujibu barua iliyoandikwa na jana Alhamisi Januari 16, 2020 na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kigoma M.R Mayunga iliuzungumzia mkutano huo wa Zitto ikisema kutokana na mazingira ya kiusalama unapaswa kusitishwa.

“Napenda kukujulisha kuwa mkutano umezuiliwa kwa tarehe uliyoomba kwa sababu za kiusalama kutokana na taarifa za kitentejensia zilizopo. Kwa hiyo hairuhusiwi kufanya au kuendelea na maandalizi ya mkutano,” ilieleza sehemu ya barua hiyo.

Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mawasiliano na Umma, Ado Shaibu amesema sababu zilizotajwa na polisi hazina mashiko na zinalenga kumzuia Zitto asitekeleze majukumu yake halali ya kuwatumikia wananchi wa jimbo hilo.

Shaibu amesema mkutano huo ulipangwa kufanyika katika viwanja vya Mwanga Center uliopo manispaa ya Kigoma Ujiji.