CCM yataka mabadiliko idadi wajumbe NEC
Muktasari:
Mwenyekiti was CCM Rais Samia Suluhu Hassan amewasilisha mapendekeo ya mabadiliko ya katiba ya chama hicho yanayotaka kuongeza idadi ya wajumbe.
Dodoma. Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Samia Suluhu Hassan amewasilisha mapendekeo ya mabadiliko ya katiba ya chama hicho yanayotaka kuongeza idadi ya wajumbe.
Katika mapendekezo hayo, CCM kinataka kuongeza wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM katika viti 15 vya Tanzania Bara na Zanzibar.
Mapendekezo hayo yamewasilishwa leo Desemba 7,2022 kwenye mkutano mkuu wa 10 wa CCM unaofanyika katika ukumbi wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma kwa lengo la kuchagua wajumbe wa Halmashauri Kuu, Mwenyekiti na Makamu Wenyeviti kwa Bara na Zanzibar.
Kwa mapendekezo hayo, idadi ya wajumbe wa NEC inaongezeka kutoka 15 hadi 20 kwa kila upande lakini nafasi za uteuzi kwa wajumbe wa NEC zinaongezeka kutoka 6 hadi 10 mabadiliko yanayotajwa kwamba yanakwenda kukiimarisha chama.
Jumlaya wajumbe 1,928 wamehudhuria mkutano huo kati ya 1,934 waliotakiwa kuhudhuria kwenye mkutano huo unaohitimisha chaguzi za CCM kwa ngazi zote kuanzia mashina hadi Taifa.
Mbali na mabadiliko hayo, CCM kinafanya mabadiliko ambapo nafasi ya katibu wa siasa na uenezi kwa ngazi ya mkoa sasa haitakuwa ya kuchaguliwa bali watateuliwa na kuwa sehemu ya ajira ingawa majukumu yao yataendelea kuwa kama ilivyo sasa.