Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Fyatu mfyatuzi sasa kugombea urahis mwaka huu wa uchaguzi

Wapendwa mafyatu wangu. Leo, rasmi nafyatua kitu. Natangaza rasmi kuwa nitakuwa kwenye debe. Naazimia kuibadili kaya kwa kufanya yafuatayo:

Mosi, nitabadili jina la kaya. Itaitwa Fyatuland na wananchi wake wataitwa mafyatu.

Hivyo, kuanzia siku nitakapoapishwa kila kitu kitabeba jina langu. Sitakuwa wa kwanza kufanya hivi.

Nenda kaulize kule Saudia. Imetokana na jina la fyatu Saudi na sasa inajinoma kwa jina lake.

Pili, nitatangaza ufalme na kufutua urahisi kwa sababu haufanyi mambo kuwa rahisi. Ili kufanya mambo rahisi, nitapiga maarufu hii domoghasia inayofanya baadhi ya mafyatu kuninyima usingizi kwa migomo hata kutishia kufanya uhasi badala ya uchanya.

Tatu, nitahakikisha mimi ndiyo nakuwa muhimili mkuu wa dola. Hivyo, bunge, mahakama, na utawala itabidi watafute pa kwenda. They’re fired.

Nne, noti na sarafu zote za kaya, vivutio vyote kuanzia mabonde, mbuga za wanyama, milima, mito, maziwa hata mashamba, viwanja vya ndege, shule na vyuo, vituo vya mbasi na treni, na kila kitu cha maana, ilikuwa na maana, vitapewa jina langu.

Kila kitu kitabeba jina langu ili kuonyesha maono, miujiza, na utukufu wangu. Pia, hii itavutia utalii na kukuza uchumi wa kaya. Pia, nitatangaza kuwa bajeti ya matanuzi na matumizi yangu ni top secret.

Tano, nitachapisha picha zangu ambazo kila fyatu atazivaa kifuani ili kumkinga na mabaya mbali na kuonyesha mapenzi makubwa kwangu, familia yangu, ukoo wangu, na maswahiba zangu.

Sambamba na hili, nitahakikisha mabango makubwa yanayoonyesha maisha yangu ya wazi siyo ya sirini kila mahali panapoonekana kwenye kaya kuanzia majumbani hadi sehemu za umma.

Hili linalenga kuniweka kwenye mioyo ya mafyatu ili wasije kufyatuka na kunifyatua.

Sita, wimbo wa taifa wa kaya utabadilika toka God bless Fyatuland kuwa God bless Fyatu Mfyatuzi na familia yake and company.

Sambamba na hili, mafyatu wataamriwa kufunga miezi mitatu kila mwaka ili kuniombea siha njema niendelee kuwatumia nitakavyo si kwa faida yangu bali yao.

Saba, nitahakikisha kila fyatu ana kadi ya kiapo cha utii na utumishi kwangu. Kadi hii itaandikwa, “hakuna Fyatu Mfyatuzi kuwatumikia mafyatu bali wao kumuabudia, kumtii, na kumtumikia kwa mioyo na roho zao zote, kwa wakati wote wa maisha yao.” Pia, nitaongeza kipengele kuwa ni kosa la jinai kutoamini kuwa kila ninachofanya ni kwa ajili ya mafyatu.

Nikila, wamekula, nikiugua, wameugua, nikitanua, wametanua, nikitumia, wametumia kwa sababu mimi ndiye alama yao kayani na duniani.

Nane, nitaanzisha vazi jipya la kaya ambalo litabeba picha yangu tukufu na ya bi mkubwa malkia.

Hii inalenga kukuza upendo na uzalendo kwa kaya yetu. Pia, itaonyesha kuwa mimi ni zaidi ya yote katika kaya na bila mimi hakuna kaya.

Au tuseme. Mimi ni kaya na kaya ni mimi na bila mimi, hakuna kaya wala mafyatu.

Tisa, viongozi wote wa dini zote za kweli na feki wataamrishwa, kila waanzapo ibada zao, kulitaja jina langu na kuniombea niishi milele mie na ukoo wangu.

Hapa lazima viongozi hao waseme kuwa mimi ni kati ya viumbe bora tangu dunia kuumbwa kuwahi kutokea.

Sambamba na hili, nitaanzisha mashindano ya kuniombea, na viongozi watakaoshinda, nawapa zawadi ima ya kuwajengea sehemu za ibada au kuwatajirisha.

Kadhalika madaktari bingwa watapaswa kupima damu yangu na kuhithibitisha ili itumike kutibu magonjwa sugu kama Ukimwi, Ukosefu wa Akili Kichwani (UAKI) na mengine mengi kama haya.

Kumi, nitatangaza sheria ya kuzuia fyatu yeyote kunikosoa, kunikashfu, kunishauri, kunishuku, kunitukana, kunikosea adabu hata kuniwazia baya. Yeyote atakayeshukiwa kufanya haya, hata kama ni ndotoni, atahukumiwa kifo anyongwe hadi afe.

Pia, hili litakuwa somo zuri kwa wengine wanaotaka kutenda kosa kubwa dhidi ya Fyatu mkubwa kama hili.

Kumi na moja, nitatangaza sheria ya kufanya kosa lolote linalohusiana na kunipinga kuwa la uhaini ili yeyote atakayefanya au kushukiwa kufanya hivyo ahukumiwe kunyongwa hadi kufa yeye, familia, na marafiki zake.

Ili kukazia, nitatangaza kijiji nilikozaliwa kwanza, kugeuzwa jiji na kuwa sehemu takatifu ya mafyatu ambapo kila mwaka watapaswa kwenda kutembelea ili kujazwa, busara, maono, na uzalendo.

Kumi na mbili, nitatangaza siku za kuzaliwa na kuingia madarakani kwangu kuwa sikukuu za kitaifa ili mafyatu wapate muda wa kusoma na kuwafundisha vitegemezi vyao historia yangu tukufu.

Historia yangu itafundishwa mashuleni kuanzia chekechea hadi PhD. Pia, kila chuo kikuu kitaamriwa kunipa PhD ya heshima na uprofesa wa kuzawadiwa. Hivyo, kuanzia siku hiyo, nitaitwa Daktari, Profesa, Muadhama, Mtukufu, Mpendwa, Mheshimiwa, Shehe, Alhaj, Ayatollah, Mullah, Ulamaa, Ustaadhi, Paroko, Askofu, Papa XVII, Mtakatifu n.k Fyatu Mfyatuzi (RIP). Naona yule anashangaa. Unadhani ulabu ni maji!!!