Karibu 2024 ila usitufyatue kama ulivyofyatukia 2023

Japo nilisherehekea kutokomea kwa mwaka 2023, machugu yake sitayasahau. Mwaka ulinifyatua sina hamu. Kuna mambo yalifanya niilaani na kuichukia 2023. Nilifyatuliwa kwelikweli.

Naamini hata mafyatu wasio wanene walifyatuliwa. Wakati sisi tukifyatuliwa, wanene walizidi kunenepa, kunenepeshana, kwa kupeana ulaji tena kwenye mgongo wetu punda wao wafyatuliwa.

Hakuna kitu kilinifyatua nikatamani mafyatu wote tuwafyatue wanaotufyatua kama tozo. Tozo kwa kila kitu hadi ukienda choo. Haya maisha gani jamani? Ukinunua au kuuza kitu, tozo. Ukifa, tozo. Nilitamani kaya yetu iitwe tozo tujue moja. Heri iwe Tanzatozo. Si inapendeza?

Wakati tukiuguza machungu ya tozo, si ukaja mgawo wa umeme. Hilo Tanesko si mnalijua lilivyo shi…pa? Mara alikuja Janwar wa Makambale akatufunga kamba na makamba kuwa mgawo wa umeme ungekuwa historia asijue utaweka historia chafu mwaka mzima.

Sijui hawa mafyatu walisomea nini na wapi. Hawajui kuwa ukiwageuza mafyatu kizani kama panyabuku wanafyatuana na kufyatua vitegemezi vingi na kuongeza umaskini kwa kaya isiyojali mafyatu wake wachovu?

Kabla ya mafyatu kutulia, si kukaja kukatikatika na kufyatuka kwa maji. Wakati dunia ikijivunia kiwango kikubwa cha maendeleo, kaya ya mafyatu inajivunia ujima! Mmejua kututenda na kututenza. Kila siku, utasikia fyatu fulani mnene akijipiga kifua kuchimba visima. Kuna visima au vyoo hasa kwa maeneo ya mjini?

Mwenzenu nimesoma hydrology kule kwenye chuo cha Fyatuology and Technology and advanced sciences. Kaya kilipo siwambii msinichimbe kama nilipewa shahada ya heshima, kughushi, au ya kununua.

Kwa ufupi, maji huko chini yamechanganyikana kwenye kitu kinaitwa water table. Hivyo, mnapofyatua visima, mnakunywa na kuogea maji ya chooni kupitia visimani. Simpo.

Hata maji ya mizoga mnayoogopa tu kuyaita maji ya mizoga. Mnajua hao wauza maji wanakoyachota? Kwa mafyatu wasivyo na huruma na ila uchu wa njuluku, unadhani watayakuta Msimbazi yaliyojaa mizoga na vinyesi wayaache wakati kuna uhaba kila wakati?

Hapa, magonjwa yatokanayo na uchafu mtayaepuka? Kwanini hawa wanaojifisifia ujinga kufanya migawo historia wakati siyo hawafyatuliwi, au kuna namna?

Kero nyingine iliyonifyatua ilikuwa ukosefu na upatikanaji ajira. Kwa wenye madingi wenye majina manene, ajira ilikuwa bwerere. Kwetu sie? We, acha tu. Wapo waliopoteza njuluku wakakopa na kusomea shahada wakati wangeweza kupata za heshima ya kutokuwa na ajira au kufanya kazi mbaya kama wale wanaopewa. Walipomaliza vyuo, ajira hakuna. Mikopo inadai. Inauma, asikwambie fyatu. 2023, niliona wengi wakitusumbua mitaani na bahasha mkononi.

Wakati wakiteseka, vichipukizi vya vigogo vilichuania ulaji. Kaya hii, we acha tu. Isipofyatuka ikafyatua wanaoifyatua tutafyatuliwa wote kutokana na ujinga na woga wetu. Acha kushangaa ndio hali halisi hiyo.

Mwaka jana nilichukia kuona vigogo wakiandaa vitegemezi vyao kuwarithi. Dingi akiwa kigogo anafyatua kagogo, akiwa jibaka anafyatua kibaka, akiwa mnene chata anafyatua chipukizi, akiwa rahisi, anafyatua waziri, na akiwa mwizi mnene anafyatua kijizi. Japo sitataja majina, 2023 ilivunja rekodi kwa kupeana ulaji kuanzia mashoga, washirika, wakwe, vitegemezi, hata wapambe kijiweni kwetu. Wakati tukipeana ulaji, mafyatu walikuwa wanafyatuliwa na matatizo usipime.

Kwetu mafyatu, kama dingi akiwa rahis, maza anakuwa rahisa, bi mkubwa anakuwa rahis dingi unakuwa rahish. Hii ni tofauti na nchi yetu isiyofuata sayansi hii.

Ukiachia hayo maumivu hapo juu, mwaka 2023 ulijaa longolongo kipolitiki. Kila aliyevuruga, alihamishiwa kwingine akavuruge zaidi. Taarifa ya ukaguzi na uthibiti wa njuluku ilifichua madudu bila hatua kufyatuliwa. Huu huitwa ulaji wa kujuana, kulindana, na kupeana.

Hizi ndizo siasa za longolongo za songombwingo wa michongo michongo. Tena kabla sijasahau, mna habari wale fyatu wasiojulikana waliofyatua na kutesa mafyatu kama vile Tunduni Lishe wamerejea? Si maneno yangu wala uzushi. Hamkuwaona wakirejeshwa kisiasa na kinamna tena kwa mbwembwe? Haya kalagabo.

Kimataifa, 2023 ilikuwa noma. Kule Sudan kwa mafyatu weusi tii wajiitao wamanga kiliumana. Maimla wawili waliwanyang’anya ulaji mafyatu walio wengi waliombandua Umar Bushir. Baada ya kufyatua madaraka si walifyatuana hadi kaya ikawaka moto hadi sasa. Mbali na huko unajua kwa wale mafyatu wanaojiona bora kuliko sote wakidai eti walichaguliwa na Maulana wakati hana ujinga huo. Yeye hata wezi na mibaka anawapa riziki wala hapendelei ingawa matapeli wengi wa kiroho wenye uroho hufundisha upuuzi huu wa mafyatu wateule.

Sitaji jina ili wanaounga uzwazwa huu mkono wasinifyatue. Si unajua mafyatu wa kaya yetu wanaopenda mambo ya hovyo na kuchukia mambo ya maana? Wakifyatuliwa Wakongomani jirani hawaandamani. Lakini hawa jamaa kikiumana, wanaandamana wakidhani wanatumikia dini zao kumbe ujuha mtupu.

Mwaka jana kule nako nao walifyatuliwa na wale waliowapora kaya yao na kuwakalia. Acha wakinukishe. Hadi sasa wafyatuliwa wameishafyatuliwa kwa maelfu na jamaa hawa waliowahi kufyatuliwa kule Uropa na jamaa mmoja ambaye naye simtaji kwa sababu za kiusalama.

Hivi nilishawatakia heri ya mwaka mpya?

Basi ndio hivyo, me nishafyatua hivyo