Mara hii mafyatu wamesahaulishwa

Kuna mbinu chafu za kuwafyatua mafyatu waufyate ili waendelee kufyatuliwa. Kilipofyatuka na kutaka kuumana kwenye sakata na sekeseke la Dip Weed, mafyatu twawala walichanganyika wakichelea kufyatuliwa.

Ili wasifyatuliwe, ilibidi wafyatue sanaa. Katika kuwafyatua mafyatu wasiwafyatue, mafyatu wanene si wakafyatua pusi toka kwenye kapu. Ghafla bin vu, ukafanyika uteuzi wa kile kijamaa kinachoghushi vyeti kilichowahi kuwika na kuzimika baada ya tamaa za ulaji kukithiri. Mwakijua, ni kibashiti. Kikiwa kimenenepeshwa na kushetasheta, si kilianza maigizo huku mafyatu wa nyuzi wakikiengaenga na kushiriki usanii wake wasijue wanafyatuliwa na kuwafyatulisha walio wengi.

Mara kitembelee huku. Mara kipande Bajaj, mara farasi, mkokoteni hadi punda ili mradi usanii uchwara. Mara kibwekee kule ili mradi sanaa. Kwa nini sauti ya wasio na sauti aka the voice of voiceless inageuzwa the voice of kipusi na chata lake?

Hapa kanusheni kuwa hamjafyatuliwa. Je, mtafyatua mafyatu wanene lini? Juzi nilikisikia kikifyatuka tena baada ya kuzimika kidogo na kuwasahaulisha mafyatu kuwa kitakwenda kutatua matatizo ya mafyatu mikoa fulani. Matatizo hayatatuliwi kwa usanii wala majukwaani bali maofisi na yalipo. Tangu lini tatizo likatatua tatizo? Kipusi chenyewe ni bomu na tatizo kubwa tu.

Kinawachonganisha na kuwadhalilisha hadi Abdi Kinamna kung’aka. Hamkusikia? Baada ya kutuliza mzuka wa Dip Weed kitakuwa wapi? Kipusi kinafyatuka kwa mamlaka hata mume wa bi Mkubwa hana. Ni kama kimetaifisha mamlaka ya Maza. Nashangaa kwa nini mwenyewe haoni hili wala hasikii. Kitakapomchafua akachafuka na kufyatuliwa atajua.

Kwa vile mafyatu ni rahisi kufyatuliwa wakafyatuka, si waliufyata na kusahaulishwa Dip Weed hadi ikazamishwa kinamna! Nani anaifyatua tena? Nani anahanikiza? Hata akina Tunda Lishu sijui Lishe, Mwabukuzi wa Mwakabuku hawasikiki na Mdude wake. Je wamefyatuliwa wakaufyata? Kunani? Kwa nini wasifufue kesi za kipusi kama kweli msemayo kuwa alitaka kuwafyatua na kuwarejeshesha namba ni ya kweli?

Kusanyeni ushahidi mkakishitaki Mahakama ya Afrika Mashariki muone kama hiki kifyatu kitaendelea kufyatua sanaa zake za sumu. Tena kwa Joji Kichaka walishakifyatua. Mkilonga nao ili mkifyatue, itakuwa rahisi.

 Je, hii geresha na hiki kifyatu uchwara vikiisha mashiko, watafyatuana? Mafyatu, jiandaeni kufyatuliwa tena kwa mara nyingine msipofyatuka na kukifyatua hiki kipusi walichokitoa kwenye kapu na waliokituma. Kimepewa ujiko na uwanja wa kufyatukafyatuka ili kuwafyatisha mafyatu wasifyatuke na kuwafyatua wanene na madudu yao kama Dip Weed.

Sasa wamanga wanachekelea baada ya kuwafyatua mafyatu kirahisi. Nangoja siku watakapoanza kuwafyatua mafyatu wetu, sijui walioingia na kuingiza hujuma hii watafyatukia wapi? Nani ajuaye? Huenda wameahidiwa pepo kule Dubei japo ni jehanam na zahama ya mafyatu fyatu wetu waliogoma kufyatuka na kufyatua.

Mie nafyatua kutimiza wajibu wangu. Kitakapoumana, nitasema nilisema lakini mafyatu hawakuelewa hadi wakafyatishwa wakaufyata. Mnauza hata banda…we koma! Heri msiniuze mie, bi mkubwa, na vitegemezi vyetu. Kweli akili ni nywele. Mnafyatuliwa na kila zoba na zwazwa nanyi msiwe mazwazwa! Mwenzenu simo na damu yenu sidaiwi. Kuna maswali muhimu ya kujiuliza na kuyafyatulia majibu sahihi haraka kabla hamjaendelea kuingizwa mkenge. Kwa nini huyu fyatu uchwara amefyatuliwa wakati wa Dip Weed ikichachamaa? Kwa nini juhudi zake zimeelekezwa kwenye kanda ya Mwendaze anayeonekana kufyatuliwa kinamna na mafyatu waliochukua ulaji baada yake kuanza kumfanya asahaulike kwa njia ya kusifiana hata pale wasipostahili?

Nangoja kuona kama ataenda Zenj na kufyatukafyatuka kabla hajafyatuliwa na mafyatu wa kule wenye historia ya kufyatuka na kuwafyatua wanene. Je, kwa nini amepewa ujiko mkubwa wakati kacheo alikotupiwa ni kadogo? Jiulize.

Yule aliyekuwapo kabla ya aliyerithiwa na haka kafyatu yuko wapi? Si alipewe unene wa wilaya? Ina maana hawa mafyatu wa chata twawala hawalijui wala kuliona hili? Who is fooling whom? Hata hivyo, wanajua wanachofanya.

Jiulize tena. Inakuwaje kifyatu chenye ulaji mdogo kama huu kiwafyatukie hata madingi wake huku kikijionyesha kila maulaji kuliko hata maza mwenyewe aliyekifyatua ili baadaye kimfyatulishe? Je, kimewazidi au watakizidi kete na kukiteketeza kama alivyofanya aliyekifyatua baada ya kumaliza kazi chafu kilichotumwa?

Kweli, mafyatu wanene wamejua kutufyatua. Yaani wanafyatua hata Mwitongo kwa Nchonga! Hamkuona kile kifimbo kikinajisiwa na hichi kifyatu uchwara? Hata hivyo, nilizoza na fyatu Mada wa Mchonga akanambia kuwa kumbe kilichotolewa ni vile vya kuchonga tu siyo kile chenyewe ambacho nimetunziwa mie kama mrithi wa kufyatuka kama alivyokuwa Mchonga.

Hata hivyo, kama mliona, mlifanya nini zaidi ya kuufyata msijue ipo siku mtafyatuliwa zaidi na zaidi muishie kunikumbuka nisiwasaidie? Kipusi aka kibashiti na mchonga wapi na wapi jamani au ni yale ya fyatu kumng’ata mbwa badala ya mbwa kumng’ata fyatu?

 Je, hizi siyo siasa chafu zaidi ya za majitaka za mwendaze Sam Six aliyekiumba hiki kipusi? Je, tumekuwa kaya ya hovyo kiasi hiki hata siri kali nzima, na ukubwa wake, kutegemea sanaa na maigizo ya kifyatu kichafu na uchwara? Heri wangenipa huo ujiko nikafyatue kila kitu bila kujali kwani mbwai mbwai. Hata hivyo, nani atampa ujiko fyatu mfyatuzi awafyatulie mbali?

Hivi sijajifyatua?