Kahata atimkia Kenya, kuzikosa mechi za Simba

Muktasari:

  • Kahata alijiunga na Simba mwanzoni mwa msimu kwa mkataba wa miaka miwili akitokea Gor Mahia ya Kenya.

Dar es Salaam. Simba itamkosa kiungo wake Francis Kahata katika michezo yao ya kirafiki kutokana na nyota huyo kuuguliwa na mtoto wake.

Simba inatarajia kucheza michezo mitatu ya kirafiki Bandari ya nchini Kenya, Mashujaa na Aigle Noir ya Burundi katika maandalizi yake ya mchezo dhidi ya Azam FC Oktoba 24 mwaka huu.

Akizungumza na Mwanaspoti, Kahata amesema yupo nyumbani kwake nchini Kenya kwa ruhusa maalumu kwaajili ya kumuuguza mtoto wake anayesumbuliwa na figo.

"Nipo Kenya nimekuja kumuuguza mtoto wangu, anaumwa figo na amelazwa katika hospitali moja huku ila anaendelea vizuri sidhani kama nitawahi michezo hiyo ya kirafiki," alisema Kahata.

Tangu kusajiliwa kwake Simba, Kahata amecheza mechi kadhaa zikiwemo mbili za Ligi ya Mabingwa hatua ya awali ambapo Simba ilitolewa na UD Songo ya Msumbiji.