Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Kane afichua kilichoiangusha England dhidi ya Argentina

Muktasari:

  • Mshambuliaji huyo amesema timu yake ilipambana kwa nguvu zote, lakini ilishindwa kufikia lengo baada ya kupoteza mchezo kwa kufungwa mabao 2-1 na Argentina.

Wakati macho ya dunia yakielekezwa kwenye fainali ya Kombe la Dunia 2026 kati ya Argentina na Hispania, nahodha wa England, Harry Kane, amevunja ukimya kufuatia kuondolewa kwa timu yake katika hatua ya nusu fainali.

Kane amefunguka hayo akieleza maumivu makubwa ya kushindwa kufikia ndoto ya kuiongoza England kucheza fainali ya kwanza ya Kombe la Dunia tangu mwaka 1966.

Mshambuliaji huyo amesema timu yake ilipambana kwa nguvu zote, lakini ilishindwa kufikia lengo baada ya kupoteza mchezo kwa kufungwa mabao 2-1 na Argentina.

Fainali ya Kombe la Dunia itachezwa Jumapili, Julai 19, 2026, katika uwanja wa MetLife uliopo New Jersey ambao kwa sasa unajulikana kama New York, New Jersey Stadium kwa ajili ya Michuano ya Kombe la Dunia  2026.

Kabla ya fainali hiyo, kutakuwa na mchezo wa kuwania nafasi ya tatu utakaozikutanisha England na Ufaransa, ambapo mataifa hayo mawili yatapambana kumaliza mashindano katika nafasi ya tatu baada ya kushindwa kuvuka hatua ya nusu fainali.

England maarufu ‘Three Lions’ ilionekana kuwa katika nafasi nzuri ya kutinga fainali baada ya kuongoza kwa bao 1-0 dhidi ya Argentina, lakini ilishindwa kulinda ushindi wa mwanzoni na kuruhusu wapinzani wao kurejea mchezoni, huku Lionel Messi akiibuka shujaa kwa kutoa pasi mbili za mabao zilizoifanya Argentina kushinda mabao 2-1 na kufuzu fainali.

Kane, ambaye ameifungia England mabao sita katika mashindano hayo, ametumia ukurasa wake wa Instagram kueleza hisia zake baada ya kipigo hicho, akisema hakuna maneno yanayoweza kueleza maumivu anayoyasikia.

Amesema England ilikuwa karibu sana kufika fainali nyingine, lakini juhudi walizoweka kwa kipindi chote cha mashindano hazikutosha kutimiza ndoto hiyo, jambo ambalo limewaacha wachezaji na mashabiki wakiwa na majonzi makubwa.

"Tulikuwa tunawapa presha kubwa na tukawa tunadhibiti mchezo vizuri. Baada ya kufunga, waliongeza mashambulizi na sisi tukashindwa kuendelea kuwabana. Mashambulizi yalikuja mfululizo na mwisho wake haikutosha,” amesema Kane.

Kane amesisitiza kuwa maelekezo ya benchi la ufundi yalikuwa ni kuendelea kushambulia hata baada ya kupata bao la kwanza.

"Ujumbe ulikuwa wazi, tuendelee kutafuta bao la pili. Lakini baada ya wao kufunga mabao mawili, hatukuweza tena kurejesha kasi ya mchezo," amesema mshambuliaji huyo.

Nyota huyo wa Bayern Munich amesema matarajio ya mashabiki kwa England yalikuwa makubwa kutokana na mafanikio ambayo timu imekuwa ikiyapata katika miaka ya karibuni, lakini bado walishindwa kuvuka hatua ya mwisho.

"Ninaelewa matarajio ni makubwa na ni sahihi kabisa. Tumekuwa tukigonga mlango wa mafanikio kwa miaka nane sasa, lakini bado tunakosa kile kipande cha mwisho cha mafanikio," ameongeza.

Katika ujumbe wake, Kane amewataka wachezaji wenzake kutumia maumivu hayo kama nguvu ya kurejea wakiwa bora zaidi.

"Sasa tunapaswa kuchukua muda kutafakari, kujifunza na kutafuta namna ya kuwa bora zaidi. Ninajivunia kila mchezaji kwa kile tulichokionyesha katika mashindano haya. Tulipitia michezo migumu na mazingira magumu, lakini tuliendelea kupambana," amesema Kane.

Ameendelea kusema kuwa safari ya kutafuta ubingwa si rahisi na mara nyingi huambatana na kuanguka kabla ya kufanikiwa.

"Kutafuta utukufu haimaanishi utaupata kila wakati. Lazima upambane, uanguke, usimame tena na kuendelea kupigania ndoto zako. Hilo ndilo tutakalofanya,” amesisitiza mshambuliaji huyo.

Nahodha huyo pia amewashukuru mashabiki waliokuwa viwanjani pamoja na wale waliokuwa nyumbani kwa sapoti waliyoitoa kwa timu katika kipindi chote cha mashindano.

"Asanteni kwa kila shabiki aliyesafiri kutuunga mkono na wale wote waliokuwa nyumbani wakituombea. Asanteni pia kwa wachezaji na benchi lote la ufundi kwa kila mlilojitoa. Kushinda au kushindwa, tutajifunza na tutarejea tena,” amesema Kane.

               

Imeandikwa na Noor Shija kwa msaada wa mtandao