Kisa kipigo Tunisia yamtimua kocha Kombe la Dunia
Taarifa zinabainisha kwamba, Shirikisho la Soka la Tunisia (FTF) limemfuta kazi aliyekuwa kocha wa timu ya taifa ya Tunisia, Sabri Lamouchi baada ya kipigo cha mabao 5-1 dhidi ya Sweden katika mechi ya kwanza ya Kombe la Dunia ya kundi F iliyochezwa alfajiri ya kuamkia leo Juni 15, 2026.
Kwa mujibu wa ripoti mbalimbali, zikiwemo za gazeti la The Guardian na mwandishi wa The New York Times, Romain Molina, Lamouchi alifutwa kazi kufuatia FTF kufanya kikao cha dharura muda mfupi baada ya kipigo hicho.
Matokeo hayo yalikuwa mwendelezo wa mfululizo wa matokeo mabaya, ikiwemo kufungwa mabao 5-0 na Ubelgiji katika mchezo wa mwisho wa kirafiki kabla ya mashindano hayo.
Ripoti kuhusu mrithi wake zinataja majina kadhaa, wakiwemo aliyekuwa winga wa Sunderland, Wahbi Khazri na Mondher Kebaier, ambaye aliiongoza Tunisia katika Kombe la Dunia 2022. Mchezo unaofuata wa Tunisia katika Kombe la Dunia utachezwa Juni 21, dhidi ya Japan.
Lamouchi mwenye umri wa miaka 54, aliteuliwa na FTF baada ya kufutwa kazi kwa Sami Trabelsi kufuatia kuondolewa Tunisia katika hatua ya 16 bora ya michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON).
Katika michezo mitano aliyosimamia, Lamouchi alianza kwa ushindi wa 1-0 dhidi ya Haiti. Hata hivyo, kikosi chake kilifunga bao moja pekee katika mechi zilizofuata, ikitoa 0-0 dhidi ya Canada kabla ya kufungwa na Austria (1-0), Ubelgiji (5-0) na Sweden (5-1).
Matokeo hayo mabaya yameonekana kuwa sababu kuu ya uamuzi wa FTF kumaliza mapema kipindi chake cha uongozi. Kwa kufanya hivyo, Sabri Lamouchi anakuwa kocha wa kwanza kufukuzwa kazi wakati Fainali za Kombe la Dunia 2026 zikiwa bado zinaendelea.