Msolla ataka wanachama kulipa ada
Aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Yanga, Mshindo Msolla, ameupongeza uongozi wa timu hiyo, huku akiwaomba wanachama kuendelea kushikamana kwa ajili ya mafanikio zaidi.
Akizungumza katika mkutano mkuu wa Yanga unaofanyika kwenye Ukumbi wa Super Dome Masaki, Msolla amesema siri ya timu hiyo kufanya vizuri ni mshikamano unaoendelea baina ya wanachama wa kikosi hicho.
"Niwashukuru uongozi uliopo madarakani kwa sasa kwa kutupa heshima kubwa ya kuwepo hapa, jambo ambalo ninawasihi wanachama wenzangu ni kushikamana na kulipa ada ili timu yetu ifanye vizuri," amesema Msolla.
Mbali na kuwa mwenyekiti Msolla ambaye kitaalamu pia ni kocha aliwahi kuifundisha klabu hiyo miaka kadhaa iliyopita.
Hivi karibuni alikuwa mmoja kati ya watu waliochukua fomu ya kuomba kugombea nafasi ya Urais ya TFF, lakini jina lake halikupitishwa.
Yanga ambao ni mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Bara, inafanya mkutano wake mkuu leo kwa mujibu wa ibara ya 20 ya katiba ya klabu hiyo ya mwaka 2021.