Mwakinyo azidi kupaa duniani

Muktasari:

  • Mpaka sasa Mwakinyo ana rekodi ya kucheza mapambano 22, ameshinda mara 20 (14 kwa (KO) amepigwa mara mbili (moja kwa KO)

Bondia Hassan Mwakinyo amepanda hadi nafasi ya 10 kwenye viwango vya ngumi za dunia katika uzani wa super welter.

Mwakinyo bondia namba moja Afrika kwenye uzani huo ameingia kwenye 'top 10' ya dunia akiachwa na mabondia tisa wanaoongozwa na Mmarekani, Jermell Charlo.

Hiyo ni nafasi kubwa zaidi kuwahi kuifikia Mwakinyo, ambaye mwaka 2018 alipanda hadi nafasi ya 14 duniani alipomchapa Sam Eggington wa Uingereza kwa Technical Knock Out (TKO).

Pambano hilo lililokuwa gumzo lilimpandisha bondi huyo hadi nafasi ya 14 duniani, ingawa baadae aliporomoka na kupanda kwa nyakati tofauti kabla y karibuni Mtandao wa ngumi za kulipwa wa dunia (Boxrec) kumtaja kwenye kuingia kwenye 'top 10'.

Boxrec imemtaja Mwakinyo kuwa namba 10 kati ya mabondia 1535 duniani kwenye uzani wake na kuendelea kuwa namba moja nchini kati ya mabondia 20 akiwa na nyota nne, akihitaji nyota moja kuingia kwenye renki ya mabondia wa nyota tano vinara wa duniani.

Pambano lake la mwisho alimchapa Julius Indongo kwa TKO na kutetea ubingwa wa African Boxing Union (ABU).