Nusu fainali sasa ni Hispania na Ufaransa
Nahodha wa Ureno, Cristiano Ronaldo akimliwaza Pepe baada ya kuondoshwa kwenye michuano ya Euro 2024 dhidi ya Ufaransa.
Muktasari:
- Mechi ya nusu fainali ya wababe hao itakuwa Jumanne Ijayo kwenye Uwanja wa Allianz Arena
Munich, Ujerumani. Hatimaye haya yanaweza kuwa mashindano ya mwisho ya mshambuliaji wa Ureno Cristiano Ronaldo baada ya jana timu yake ya taifa ya Ureno kutupwa nje na Ufaransa kwa mikwaju ya penalti.
Ronaldo mwenye miaka 39 juzi aliiongoza Ureno akitafuta ubingwa wake wa pili wa michuano hiyo mikubwa Ulaya lakini mechi hiyo ilimalizika dakika 120 kwa suluhu na mikwaju ya penalti ikaitupa Ureno nje.
Staa wa Ureno Joao Felix ndiye pekee alipoteza mkwaju wa penalti huku mastaa wengine wote wakifunga na Ureno kwenda nje kwa penalti 3-5.
Ureno ilifunga penalti zake kupitia kwa Cristiano Ronaldo, Nuno Mendez na Bernado Silva, huku Ufaransa iliyotinga nusu fainali ikifunga kupita kwa Theo Hernandez, Brandle Barcola, Youssouf Fofana, Jules Kounde na Ousmane Dembele.
Sasa Ufarasa inatarajiwa kuvaana na Hispania ambayo ilifanikiwa kuwatupa nje Wajerumani kwa kuwachapa mabao 2-1 kwenye mchezo mwingine uliokwenda hadi dakika 120.
Hispania, ambayo awali ilikuwa haipewi nafasi kubwa ya kuibuka na ushindi ilianza kufunga kupitia kwa Dani Olmo dakika ya 51, lakini Ujerumani ikasawazisha kwa bao safi liliwekwa kimiani na Florian Wirtz katika dakika ya 89 ya mchezo huo.
Wakati mashabiki wakiamini kuwa mechi hiyo inakwenda kwenye matatu, Mikel Merino aliwashangaza wengi baada ya kufunga bao safi katika dakika 119 na kuipeleka timu hiyo hatua ya nusu fainali.
Mechi ya nusu fainali ya wababe hao itakuwa Jumanne Ijayo kwenye Uwanja wa Allianz Arena.