Okwa: Bado Yanga

KIUNGO mpya wa Simba, Nelson Okwa amewaambia Yanga, “bado nyie.” Staa huyo ametuma salamu kwa watani zao akisema kile alichoonyesha kwenye kilele cha tamasha la Simba Day juzi Jumatatu ni mfano tu.

Katika tamasha hilo, Simba ilicheza mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya mabingwa wa Ligi Kuu ya Ethiopia, St George ambapo ilishinda mabao 2-0 huku moja likifungwa na nyota huyo raia wa Nigeria.

Katika mchezo huo uliochezwa Uwanja wa Mkapa, Okwa alionyesha kiwango bora hasa mikimbio na pasi za haraka haraka.

Simba na Yanga zitakutana katika mchezo wa Ngao ya Jamii utakaochezwa Jumamosi hii katika Uwanja wa Mkapa ambapo ni lazima timu moja ishinde ili apatikane bingwa wa mechi hiyo ya ufunguzi wa Ligi Kuu Bara itakayoanza rasmi Agosti 15, mwaka huu.

Akizungumza na Mwanaspoti, Okwa alisema: “Nilichoonyesha ni mfano tu kwa mashabiki wa Simba. Nadhani nitakuwa kwenye kiwango bora muda si mrefu ligi ikianza hadi mwisho wa msimu,” alisema Okwa ambaye ameonyesha ana kitu mguuni kwake kitakachoisaidia Simba inayoanzia hatua ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika. Wachezaji wengine waliosajiliwa Simba ni Nassor Kapama, Habibu Kyombo, Agustine Okrah, Victor Akpan, Moses Phiri, Mohamed Outtara na Dejan Georgijevic.