Phiri, Bocco wote freshi tu

ACHANA na maneno ambayo yanaendelea huko mitaani, katika vijiwe vya soka ikiwemo vile vya kidigitali kuwahusu wachezaji watatu wa Simba waliopo huku kambini Misri.

Wachezaji hao ni nahodha John Bocco, Shomary Kapombe na Moses Phiri kuwa wanaumwa na watakosa baadhi ya michezo kuanzia ule wa Simba Day hilo si la kweli kwani mashine hizo zipo fiti zinaendelea na mazoezi kila siku asubuhi na jioni.

Bocco, Kapombe na Phiri wamekuwa wakifanya kila zoezi ambalo makocha wa Simba wamekuwa wakuwapatia kulingana na ratiba na wamefanya bila kukosa.

Wakati huo huo Bocco na Phiri wameonekana kuwa na maelewano mazuri na wamekuwa wakitengenezeana nafasi za kufunga mara kwa mara.

Phiri alikuwa akitoa mapande mengi kwa Bocco ambaye jukumu lake lilikuwa ni kuweka kambani na wala hilo halikuwa shida kwani alionekana kuimarika kwa kufunga mabao mengi.

Wakati huo huo kama kawaida yake Kapombe alikuwa imara katika kuzuia mashambulizi na kupiga mitungi ya maana kwa washambuliaji kama ule aliompigia Pape Sakho dhidi ya Asec Mimosas na kufunga Bao Bora la CAF ngazi ya klabu msimu uliyomalizika.

Phiri alisema yupo fiti kwa asilimia zote ndio maana anaendelea na mazoezi ya kila siku huku akifanya vizuri kulingana na kazi anayotakuwa kuifanya.

Alisema tangu amefika Simba wachezaji wapya na wale waliokuwepo msimu uliopita kumekuwa na ushindani wa kutosha kwao na hilo ni jambo zuri kwani ni moja ya silaha yao kufanya vizuri.

“Lazima tushindane kwanza ndani ili kila mmoja akifanya vizuri maana yake timu itafanikiwa katika kila mechi. Wote tupo sawa hadi wakati huu, unaangalia mazoezi hapa si unaona tupo na morali ya kuhakikisha malengo yanatimia,” alisema Phiri aliyesajiliwa na Simba msimu huu akitokea Zanacco ya Zambia.