PSG yafanya kufuru usajili wa Messi
Muktasari:
- Klabu ya Paris Saint Germain, imekamilisha usajili wa aliyekuwa nahodha na mfungaji bora wa muda wote wa FC Barcelona, Muajentina, Lionel Messi, ambaye alimaliza mkataba wake Juni, mwaka huu ndani ya timu hiyo.
Klabu ya Paris Saint Germain, imekamilisha usajili wa aliyekuwa nahodha na mfungaji bora wa muda wote wa FC Barcelona, Muajentina, Lionel Messi, ambaye alimaliza mkataba wake Juni, mwaka huu ndani ya timu hiyo.
Ikumbukwe kuwa, Messi, alikuwa amekubali kusaini dili jipya la kuendelea kuitumika Barcelona, lakini dili hilo lilishindwa kukamilika kutokana na sheria ya matumizi ya fedha ambayo iliwataka Barcelona kupunguza mishahara au kuuza baadhi ya mastaa wake kwa ajili ya kuweza kumsajili Messi.
Baada ya dili hilo kushindwa kukamilika, tayari PSG imekamilisha usajili wa nyota huyo ambaye amesaini mkataba wa miaka miwili ya kuitumikia timu hiyo, huku kukiwa na kipengele cha kuweza kuongeza mwaka mmoja baada ya mkataba wa awali kumalizika.
Dili hilo lina thamani ya pauni milioni 35 kwa mwaka, litamfanya Messi alipwe mshahara wa pauni milioni moja kwa wiki, ingawa kutokana na makato itamlazimu Messi kupokea pauni 625,000, kwa wiki.
Agosti 10, mwaka huu, PSG ilimtambulisha nyota huyo na leo atakuwa kwenye dimba la Parc des Princes kwa ajili ya kutambulishwa kwa mashabiki wa timu hiyo ambayo maskani yake ni jijini Paris.