Salah aiokoa Misri ikiichapa Zimbabwe
Muktasari:
- Misri na Afrika Kusini zinaongoza msimamo wa kundi B, kila moja ikiwa na pointi tatu, ikifunga mabao mawili na kufungwa moja.
Mohamed Salah amefunga bao katika dakika za majeruhi kuipa Misri ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Zimbabwe katika mchezo wa Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) uliochezwa Jumatatu, Januari 22, 2025 katika Uwanja wa Adrar jijini Agadir, Morocco.
Prince Dube alianza kuwashtua Misri kwa kuifungia Zimbabwe bao la kuongoza katika dakika ya 20 lakini Misri walisawazisha katika dakika ya 64 kupitia kwa Omar Marmoush.
Iliwalazimu Misri kusubiri hadi katika dakika za nyongeza kupata bao la pili kupitia kwa Salah ambalo limewapa mwanzo mzuri kwenye fainali hizo mwaka huu.
Jijini Marrakech, Afrika Kusini ‘Bafana Bafana’ ilianza vyema mashindano hayo kwa kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Angola.
Oswin Appolis alianza kuifungia bao la kuongoza Bafana Bafana katika dakika ya 21, na lilidumu kwa dakika 14 tu kwani katika dakika ya 35, Angola walisawazisha kupitia kwa Show.
Lyle Foster aliwainua vitini mashabiki wa Afrika Kusini katika dakika ya 79 baada ya kuifungia timu yake bao la pili ambalo liliihakikishia ushindi Bafana Bafana.
Jijini Casablanca kwenye Uwanja wa Mohammed V, bao la dakika za majeruhi la Patson Daka wa Zambia liliinyima fursa Mali ya kuibuka na ushindi katika mchezo huo ambao ulimalizika kwa sare ya bao 1-1.
Ilionekana kama Mali ingeibuka na ushindi katika mechi hiyo baada ya kutangulia kupata bao kupitia kwa Lassine Sinayoko katika dakika ya 61 lakini bao la Daka liliiokoa Zambia na kuipa pointi moja kwenye mchezo huo.