Sarpong anauzwa, inaletwa mashine nyingine Yanga

Sarpong anauzwa, inaletwa mashine nyingine Yanga

Muktasari:

  • Yanga ilimtaka, Idris Mbombo raia wa DR Congo aliyekuwa akiichezea Nkana, lakini ikachemka dakika za mwisho kwa kushindwa kufikia dau lake akaibukia El Gouna ya Misri.

YANGA wapo kwenye mchakato wa kumuuza straika wao, Michael Sarpong kabla ya kufungwa kwa dirisha dogo wikiendi ijayo. Dili hilo wanakimbizana nalo kwa haraka ili wakamilishe usajili wa straika Mkongomani ambaye nae kila kitu kinakwenda vizuri baada ya kushindwana na Idris Mbombo aliyetimkia Misri.

Lakini mbali na dili hilo, pia Yanga wako kwenye mchakato wa kumpata straika tegemeo wa Mbeya City, Kibu Denis. Kibu ambaye ana mkataba wa mwaka mmoja na nusu ameitumikia Mbeya City nusu msimu, hivyo Yanga itawalazimu kuingia mfukoni kufanya mambo.

Licha ya kwamba Yanga wanafanya siri kubwa, lakini habari za uhakika ambazo Mwanaspoti limezipata jana mjini hapa ni kwamba itamuachia Sarpong baada ya kupata dili la kucheza nje, hivyo wanataka kutumia nafasi hiyo kufanya mabadiliko kikosini kabla dirisha halijafungwa Jumamosi ijayo kwa kusaini Mkongomani ambaye Cedrick Kaze anacheki na wakala wake.

Awali, Yanga ilimtaka, Idris Mbombo raia wa DR Congo aliyekuwa akiichezea Nkana, lakini ikachemka dakika za mwisho kwa kushindwa kufikia dau lake akaibukia El Gouna ya Misri. Lakini pia wako kwenye mazungumzo na straika mmoja wa Ivory Coast, Gbagbo Junior ingawa vilevile jana ilielezwa kwamba baadhi ya wanakamati wameshauri klabu iachane naye. Kuhusu Kibu, Mbeya City wamedai hauzwi.