Serikali mbioni kuirejesha Ligi ya Muungano

Naibu Waziri wa Sanaa, Michezo na Utamaduni, Hamis Mwinjuma 

Muktasari:

  • Naibu Waziri amesema pande mbili zimeshakutana na kujadiliana namna wanavyoweza kuirudisha ligi hiyo.

Dodoma. Serikali iko mbioni kurudisha Ligi ya Muungano lakini imetoa sababu ya kukosa ufadhili kwamba limekuwa ni tatizo.

Kauli hiyo imetolewa bungeni leo Alhamisi Novemba 2, 2023 na Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma wakati ajibu swali la nyongeza la Mbunge wa Magomeni (CCM) Mwanakhamisi Kassim Said.

Kwenye swali la msingi mbunge huyo ameuliza ni lini Serikali itarudisha mashindano ya ligi ya Muungano ambayo ilikuwa ni kivutio na hamasa katika kuibua vipaji.

Katika swali la msingi mbunge huyo ameuliza TFF inashirikianaje na ZFF kupandisha hadhi ligi ya Zanzibar na kuendeleza vipaji vya wachezaji wa Zanzibar.

“Serikali ipo kwenye mchakato wa kurudisha Ligi ya Muungano na mapema tutairudisha, tatizo litakuwa kwenye udhamini kwani ndiyo kitu tunachokitafuta kwa sasa,” amesema Mwinjuma.


Akijibu swali la msingi, amesema Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) chini ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imekuwa ikishirikiana na ZFF katika mipango mbalimbali kwa lengo la kuendeleza Soka la Tanzania.

Naibu Waziri amesema kwa sasa Bodi ya Ligi ipo katika mchakato wa kuandaa mafunzo ya uendeshaji wa Bodi ya Ligi ya Zanzibar ambayo kimsingi yatalenga namna ya uendeshaji wa Bodi ya Ligi katika masuala ya Menejimenti, Ligi na masuala ya uwekezaji, udhamini na masoko.

Naibu Waziri amesema kwa upande wa kuibua vipaji, TFF imekuwa ikishirikiana na ZFF katika uteuzi wa wachezaji katika timu za Taifa za vijana, ambapo vijana kutoka Zanzibar wamekuwa wakiitwa katika vikosi vya timu ya Taifa ya vijana na hatimae kucheza katika timu ya Taifa ya wakubwa Taifa Stars.