Simba yatambulisha mrithi wa Manara

Ofisa Habari na Mawasiliano mpya wa Simba, Ahmed Ally

Muktasari:

Kabla ya leo kutambulishwa kuwa Ofisa Habari na mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally alikuwa mtangazaji na mzalishaji wa vipindi katika kituo cha habari cha Azam.

ASUBUHI ya leo klabu ya Simba imemtangaza Ahmed Ally kuwa Mkuu wa idara ya Habari na Mawasiliano mpya wa timu hiyo.

Ahmed ambaye kabla ya kutambulishwa leo, alikuwa mtangazaji na mzalisha vipindi wa kituo cha habari cha Azam Media na ameenda Simba kuchukua nafasi iliyoachwa na Haji Manara tangu Julai 28, 2021.

Baada ya Simba kuachana na Manara ambaye siku chache baadae alitimkia kuwa Msemaji wa Yanga, ilimteua Ezekiel Kamwaga kukaimu nafasi hiyo kwa kwa kipindi cha miezi miwili.

Baada ya Kamwaga kumaliza muda wake wa kukaimu, kiti hicho hakikuwa na mtu hadi leo alipotambulishwa Ahmed kupitia mitandao rasmi ya klabu hiyo.

Katika utambulisho wake, kwenye kurasa Instagram ya Simba, kuliandikwa maneno ya ukaribisho yakisomeka hivi;

“Ni kijana mchapakazi, mwenye uhusiano mzuri na watu wa aina zote, mtanashati na kubwa zaidi mapenzi yake kwa Simba hayapimiki.

Ahmed Ally, karibu kwenye klabu ya maisha yako kuwatumikia Wanasimba kama Afisa Habari na Mawasiliano.”