Taifa Stars, Niger zapishana dakika tano Zanzibar
Muktasari:
- Taifa Stars inashika nafasi ya pili kwenye msimamo wa kundi E la kuwania kufuzu Kombe la Dunia 2026 ikiwa na pointi 10.
Zanzibar. Timu za taifa za Tanzania ‘Taifa Stars’ na Niger zimepishana kwa dakika tano katika uingiaji wa kwenye eneo la kuchezea la Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar kwa ajili ya kupasha miili joto.
Mechi hiyo ya leo ni ya kundi E ikiwa ni ya kuwania kufuzu Fainali za Kombe la Dunia 2026 ambayo inachezwa kuanzia saa 10:00 jioni, leo Septemba 9, 2025.
Wachezaji wa Taifa Stars wameingia kiwanjani saa 9:16 alasiri na baadaye Niger wakaingia saa 9:21.
Wakati Taifa Stars inaingia uwanjani, mashabiki waliojitokeza uwanjani hapa waliwashangilia ambapo wachezaji nao wakapiga makofi ya kuwashukuru.
Sauti na makofi yaliongezeka zaidi baada ya kocha msaidizi Juma Mgunda kutoka nje ya vyumba vya kubadilishia nguo na kuwapungia mashabiki huku akiwapigia makofi.
Taifa Stars iliyo nafasi ya pili katika kundi E inaingia katika mchezo wa leo ikiwa na pointi 10 ambazo imekusanya kwa kupata ushindi katika mechi tatu, kutoka sare moja na kupoteza moja.
Niger ina pointi sita na inashika nafasi ya nne katika msimamo wa kundi hilo linaloongozwa na Morocco ambayo tayari imeshafuzu Kombe la Dunia.
Kumbukumbu zinaonyesha Taifa Stars imekuwa na historia nzuri katika michezo yake dhidi ya Niger ambapo katika mechi tatu walizokutana, imepata ushindi mara mbili na kutoka sare moja.
Lakini pia Taifa Stars inaingia katika mechi ya leo ikiwa na mwenendo mzuri kulinganisha na wapinzani wao Niger.
Katika mechi sita zilizopita hivi karibuni, Taifa Stars imepata ushindi mara tatu, imetoka sare mbili na kupoteza moja tu.
Niger yenyewe katika mechi sita zilizopita, haijapata ushindi na imetoka sare tatu huku ikipoteza mechi tatu.