Yanga yapewa mbinu

Yanga yapewa mbinu

Muktasari:

  • YANGA itaanza Ligi Kuu Tanzania Bara na Kagera Sugar ugenini Septemba 27 na imepewa mbinu itakayowapa morali mastaa wapya, kuhakikisha wanaanza na kiwango cha juu katika mechi za mwanzo.

YANGA itaanza Ligi Kuu Tanzania Bara na Kagera Sugar ugenini Septemba 27 na imepewa mbinu itakayowapa morali mastaa wapya, kuhakikisha wanaanza na kiwango cha juu katika mechi za mwanzo.

Nyota wa zamani wameibuka na kuwapa mbinu za kuwafanya wachezaji waanze vizuri msimu na zitakazowafanya wajiamini.

Straika wa zamani wa timu hiyo, Mkongomani David Molinga alisema mastaa waliopo tangu msimu uliopita wanapaswa kuwa wahamasishaji kwa wale wageni ili kuwajengea morali ya kupambana na hiyo itasaidia kwenda nao sawa na kufanya kile kinachosubiriwa na mashabiki wa timu hiyo.

“Yanga kuna wachezaji wazoefu wanaotakiwa kuongoza kuhamasisha wengine ili kuingia kwenye mifumo ya timu, naamini wanaweza wakaanza kwa ushindi, ingawa ligi ni ngumu inahitaji kupambana zaidi,” alisema ambaye ametua Namungo FC msimu huu.

Naye beki wa timu hiyo, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ alisema wanajipanga kuhakikisha wanapigania timu yao, kuanza na ushindi utakaowasaidia kujenga misingi mizuri ya morali na ujasiri.

“Matokeo mazuri yanaleta hamu ya kupambana na ndio maana kuna haja ya kuendelea kuhamasishana kuona tunafungua dimba kwa nguvu zote,” alisema Ninja. Naye Kocha wa Kagera Sugar, Francis Baraza alisema licha ya baadhi ya wachezaji kuchelewa kuingia kambini, anawajenga kuanza kwa kupata ushindi mchezo wa kwanza utakaowafungulia baraka za kuwa bora msimu huu.

“Kwa sasa nafanya kazi mbili. Ya kujenga fitinesi na kombinesheni ya wachezaji ili kuhakikisha natengeneza kikosi cha kucheza kitimu ili tukianza mechi ya kwanza tushinde,” alisema.