ZA NDAANI KABISA: Mnigeria mbioni kusepa Simba

HUKO mtaani kwa sasa mjadala wa straika wa Simba, Dejan Georgijevic ‘Mzungu’ kuamua kujiengua ghafla kikosini kwa tuhuma za kukiukwa kwa baadhi ya vipengele vya mkataba wake na klabu hiyo ya Msimbazi, lakini Za Ndaani Kabisa zinasema nyota mwingine yupo mbioni kusepa.

Chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya Simba, kimedai kuwa Mnigeria, Nelson Okwa hana furaha Msimbazi na huenda akatimka klabuni hapo katika dirisha dogo. Okwa ambaye bado hajawakuna mashabiki wa Simba tangu atue msimu huu akitokea Rivers United ya Nigeria, inadaiwa hana furaha na kama mambo yataendelea huenda dirisha dogo likamrudisha kwao, japo itategemea na upepo utakavyokuwa baina yake na mabosi wa klabu hiyo.

“Kuna hali ambayo haimfurahishi ndani ya timu, lakini hata kiwango chake ni tofauti na alivyokuwa Rivers Utd, kuna uwezekano katika dirisha dogo akasepa ama kusepeshwa,” chanzo hicho kilisisitiza na kuongeza hata mashabiki wa Simba ni kama hamuelewi ukilinganisha na alivyokuwa Mzungu.

Mshambuliaji huyo hadi sasa amefunga bao moja tu kwenye mechi ya Tamasha la Simba Day lililofanyika Agosti 8 na Simba kuifumua St George ya Ethiopia kwa mabao 2-0, huku akiwa hajapata namba kwenye kikosi cha kwanza cha timu hiyo tangu timu ikiwa chini ya Kocha Zoran Maki.

Awali ilielezwa Kocha Zoran aliyetimkia Al Ittihad ya Misri, hakumkubali Okwa na aliwahi kumpasha live kama alivyowafanyia baadhi ya nyota wake akiwamo Clatous Chama, lakini tangu Simba iwe chini ya Juma Mgunda ameanza kupewa nafasi ya kucheza japo hajaonyesha makali yaliyotarajiwa na wengi.