Madai wasichana kuolewa kinguvu yashika kasi Pakistan
Wahanaharakati wa haki za binadamu nchini Pakistan wamezitaka mamlaka nchini humo kukomesha matukio ya utekaji wa wasichana wanaoozeshwa na wengine kulazimishwa kubadili dini bila ridhaa yao.
Wameeleza hayo katika mkutano wao na waandishi wa habari, wakisisitiza kuwa mamlaka zinatakiwa kuchukua hatua ili kuondoa hofu katika jamii.
‘’Wiki iliyopita msichana mmoja mkazi wa Gulbahar alikamatwa na kuozeshwa bila ridhaa yake. Baba mzazi wa binti huyo, Abbas Masih aliwahoji polisi na kuelezwa kuwa binti yake alifunga ndoa kwa ridhaa yake,’’
"Tulishtuka kuona cheti cha ndoa tena kikionesha kuwa alibadili dini pamoja na taarifa kutoka mahakamani, hili suala ni kati ya mambo mengi yanayowakuta wasichana wadogo,’’ alisema Mohammed Liaqat wakati akisoma tamko la wanaharakati hao, akisisitiza kuwa wanaofanyiwa ukatili huo ni wasichana wenye umri wa miaka 12 hadi 17.
Hata hivyo, madai hayo yamekanushwa na mamlaka nchini Pakistan zikibainisha kuwa matukio yote yanayotokea, huripotiwa na wahusika kuchukuliwa hatua, ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani.
Madai hayo yametolewa wakati ambao ripoti ya orodha ya waangalizi wa dunia ya Open Doors ya 2026 ikionesha Pakistan kuwa miongoni mwa nchi ambazo bado wasichana wanaolewa wakiwa na umri mdogo, kupendekeza umri kuanzia miaka 18.
Pia, tume ya watu ya haki za wachache inayotetea, kulinda na kukuza haki za jamii za watu wachache nchini humo ilipendekeza kuhusu matukio hayo ya wasichana kuozeshwa na kutaka sheria kubadilishwa.
‘’Watoto hawa hutekwa nyara, hupewa dawa za kulevya, hutishiwa na kulazimishwa kuingia kwenye ndoa lakini hata kesi zikienda mahakamani hatuoni haki ikitendeka kama matarajio yalivyo katika jamii,’’ alidai Liaqat.