Mahakama yaiamuru Serikali kurekebisha kifungu Sheria ya Mtandao

Muktasari:

Uamuzi huo umetolewa na Mahakama Kuu,umeipa Serikali miezi 12 kukifanyia marekebisho kifungu cha 50 cha Sheria ya Makosa ya Mtandao kilichobatilishwa.

Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) ameondolewa mamlaka ya kutoa adhabu isiyokatiwa rufaa kwa mshtakiwa anayekiri makosa ya kimtandao.

Uamuzi huo umetolewa na Mahakama Kuu,umeipa Serikali miezi 12 kukifanyia marekebisho kifungu cha 50 cha Sheria ya Makosa ya Mtandao kilichobatilishwa.

Hata hivyo, mahakama hiyo imehalalisha vifungu vingine vyote vya sheria hiyo, ambavyo pia vimekuwa vikilalamikiwa na wadau wa matumizi ya mitandao na teknolojia ya habari.

Uamuzi huo umetokana na kesi ya kikatiba, iliyofunguliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), Kituo cha Msaada wa Sheria na Haki za Binadamu (LHRC)na mashirika mengine.

Katika hukumu iliyotolewa na majaji Profesa John Ruhangisa, Winfrida Korosso na Lugano Mwandambo, Mahakama ilibatilisha Kifungu cha 50 cha sheria hiyo, lakini ikaridhia vingine kuwa ni halali.