Diamond aeleza sababu za kuachana na Vevo

Muktasari:

  • Neno Hallelujah limetumika kama kionjo cha kusifu uumbaji wa Mungu na si kama wengi wanavyotafsiri

Dar es Salaam. Mwanamuziki Diamond Platnumz amelitolea ufafanuzi suala la mtandao wa YouTube na Vevo baada ya kuzuka sintofahamu kuhusiana na chaneli hizo mbili za kurushia nyimbo za wasanii.

Katika maelezo yake pia ametoa sababu za kuuita wimbo Hallelujah alioutoa juzi usiku. Wimbo huo uliowekwa saa 38 zilizopita umetazamwa na watu milioni1.6 katika mtandao wa YouTube.

Diamond amesema licha ya kujiunga na mtandao wa Vevo, aliamua kuachana nao kutokana na masuala ya maslahi kutomridhisha.

Amesema kulinganisha YouTube na Vevo kwa mtu anayejua masuala ya mitandao ni sawa na kulinganisha baba na mtoto.

“Vevo wanauza Youtube hivyo moja kwa moja mtandao ninaoutumia kuweka kazi zangu ndiyo ambao unanilipa zaidi na ndiyo mtandao mama, ni kweli niliingia Vevo hapo awali lakini kutokana na kushidwana kwenye maslahi niliamua kuachana nao,” amesema mwanamuziki huyo.

 

 Kwanini alitumia neno Hallelujah?

 

Meneja wa mwanamuziki huyo, Salaam Sharaf amesema jina la wimbo huo limetumika kama kionjo cha kusifu uumbaji wa Mungu na si kama wengi wanavyotafsiri.

 

Salaam hakuishia hapo alitolea mifano ya baadhi ya wasanii hapa nchini ambao wamewahi kuweka neno Mashaalah katika nyimbo zao, huku wengine wakitumia neno Halelluya maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi akiwemo mwanamuziki Nameless katika wimbo wake “Nasinzia”.

 

“Wakati anatunga mashairi yake lengo lilikuwa kusifia uumbaji, mbona wapo wasanii wengi hapa nchini wametumia neno Mashaallah, Hallelujah maana yake ni kumtukuza na kumsifu Mungu lina tofauti gani na Mashaalah?” amehoji Salaam.

 

Hata hivyo amesema watu wanaozungumzia suala hilo wanatafuta namna ya kuonekana wanaongea na iwapo wanaona kuna mahali mambo hayajakaa sawa ni vema wakaenda kwenye vyombo vya sheria, “Nafikiri hawana jipya wameshindwa watasema nini kuhusu wimbo huu, hawana sababu ya msingi.”