Meya wa Jiji Dar aachiwa kwa dhamana

Muktasari:

Baada ya kumshikilia kwa zaidi ya saa 24, Polisi imemuachia kwa dhamana Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita


Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limemuachia kwa dhamana Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita baada ya kumshikilia kwa zaidi ya saa 24.

Mwita ambaye ni diwani wa Vijibweni (Chadema) alikamatwa na polisi juzi Desemba Mosi, 2018 saa 11 jioni baada ya kumaliza kikao cha kutunisha mfuko wa vijana na kuachiwa jana saa 2 usiku akituhumiwa kufanya maandamano bila kuwa na kibali.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumatatu Desemba 3, 2018 wakili wa Meya huyo, Alex Massaba amesema baada ya polisi kuchukua maelezo walimuachia kwa dhamana na kumtaka aripoti leo kwa mkuu wa upelelezi Wilaya ya Kigamboni.

“Mteja wangu amepata dhamana jana saa mbili usiku baada ya kuhojiwa kwa kosa la kufanya maandamano bila kibali na kutakiwa kuripoti kwa mkuu wa upelelezi wilaya ya Kigamboni leo,” amesema Massaba.

Katika maelezo yake ya jana Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema Mwita alikamatwa kwa kosa la kuongoza maandamano bila kutoa taarifa polisi.