TBA yafanya uchunguzi picha zilizozagaa mtandaoni

Muktasari:

  • Majengo ya hosteli hizo yalijengwa na TBA kwa miezi minane yakielezwa kugharimu Sh10 bilioni.

Dar es Salaam. Wakati picha za majengo yenye nyufa zikisambaa mitandaoni ikidaiwa ni ya hosteli mpya za Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), uongozi wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) umekwenda kukagua ili kujiridhisha.

Majengo hayo yaliyojengwa na TBA kwa miezi minane yakielezwa kugharimu Sh10 bilioni yalizinduliwa Aprili 15,2017.

Ujenzi ulifanyika ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais John Magufuli la kumaliza tatizo la malazi kwa wanafunzi wa UDSM.

Akizungumza na MCL Digital leo Jumapili Desemba 3,2017 Ofisa Mtendaji Mkuu wa TBA, Elius Mwakalinga amesema hata yeye ameziona picha hizo kwenye mitandao ya kijamii.

“Nimeziona na muda huu najiandaa kwenda huko kuangalia kama taarifa hizo ni za kweli,” amesema Mwakalinga alipozungumza na MCL Digital saa mbili usiku. Picha hizo zilianza kusambaa leo jioni.

Mwakalinga amesema huenda picha hizo ni za majengo mengine lakini zimehusishwa na hosteli hizo.

“Nitatoa taarifa baada ya kukagua majengo hayo kwa sasa siwezi kuzungumza hadi nitakapoona,” amesema.