Waliokuwa vigogo Tanesco wapandishwa Kisutu
Dar es Salaam. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imewafikisha mahakamani vigogo watano wa zamani wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na msambazaji kutoka kampuni ya M/S Young Dong Electronic Co. Ltd, kwa tuhuma za uhujumu uchumi kwa kuisabishia Serikali hasara ya Sh 275 milioni.
Vigogo hao ni Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, Robert Shemhilu, Ofisa Ugavi, Harun Mattambo, Mkurugenzi wa Fedha, Lusekelo Kasanga, mwanasheria wao, Godson Makia pamoja na msambazaji Martin Simba.
Leo Alhamisi washtakiwa hao walisomewa mashtaka mawili yanayowakabili ya uhujumu uchumi ikiwamo matumizi mabaya ya madaraka na kusababisha hasara mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu,Thomas Simba.
Wakili wa Serikali Mkuu, Vitalis Peter alidai kati ya Januari na Desemba 2011 katika ofisi za Tanesco Ubungo, washtakiwa wakiwa waajiriwa wa shirika hilo, walitumia madaraka yao vibaya kwa kufanikisha malipo kwa msambazaji Martin Simba bila ya kufanya uhakiki.
Vitalis alidai kuwa walifanya hivyo kinyume na kifungu cha 35 cha Sheria ya Manunuzi ya Umma namba 21 ya 2014 kitendo ambacho kilisababisha msambazaji huyo kupata faida.
Aliendelea kudai kuwa kati ya Januari na Desemba, mwaka 2011 katika ofisi za Tanesco Ubungo, washtakiwa hao wakiwa waajiriwa wa shirika hilo pamoja na msambazaji huyo waliisababishia Serikali hasara ya Sh 275,040,000.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo washtakiwa waliruhusiwa kuongeza kwa sababu Mkurugenzi wa Mashtaka DPP aliwasilisha cheti maalum kilichoiruhusu Mahakama kuisikiliza kesi hiyo.
Hivyo walikana na upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi umekamilika.
Washtakiwa hao watasomewa maelezo ya awali (PH) Agosti 24,2017.