Kakolanya arejea golini, Aussems apangua kikosi

Muktasari:

Kakolanya hakuweza kucheza mchezo wowote wa Ligi Kuu mbele ya Aishi Manula lakini katika mchezo huu wa kirafiki, kocha Patrick Aussems amemuanzisha kuwaongoza wenzake.

KIPA Beno Kakolanya wa Simba, amerejea katika kikosi cha kwanza cha klabu hiyo kitakachocheza mchezo wa kirafiki wa kimataifa leo Jumamosi saa 10 dhidi ya Bandari FC Kenya, mechi hiyo itachezwa uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Mara ya mwisho Kakolanya kucheza kikosi cha kwanza ni mchezo wao wa Simba Day na ule wa kwanza Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Ud Songo, baada ya hapo Aishi Manula ndiye alikaa langoni muda wote.
Kakolanya hakucheza mchezo wowote wa Ligi Kuu mbele ya Manula lakini katika mchezo huu wa kirafiki, kocha Patrick Aussems amemuanzisha kuwaongoza wenzake.
Katika kikosi hicho Aussems amewaanzisha nyota wengi ambao hawajapata nafasi ya kuanza kikosi cha kwanza ambapo upande wa beki ya kulia amemuanzisha Haruna Shamte ambaye mara nyingi nafasi hiyo huchezwa na Shomari Kapombe.
Kwa upande wa beki ya kushoto amemuanzisha chipukizi Joseph Peter na kumpumzisha nahodha wake Mohamed Hussein 'Tshabalala' huku safu zingine zikiwa na nyota wake wale wale.
Kikosi kilivyo, Beno Kakolanya, Haruna Shamte, Joseph Peter, Tairone Santos, Pascal Wawa, Gerson Fraga, Deo Kanda, Sharaf Shiboub, Wilker Da Silva, Ibrahim Ajibu na Francis Kahata.
Wachezaji wa benchi, Aishi Manula, Athumani Mtamilwa, Yusuph Mlipili, Kennedy Juma, Said Ndemla, Maulid Lembe, Salum Shaban, Rashid Juma, Andrew Michael na Dickson Mhilu.