Rose Muhando amerudi upya kwenye muziki

MWIMBAJI wa nyimbo za Injili, Rose Muhando ameibuka na kutoa wimbo mpya uitwao Walionicheka ambao unatamba kwasasa kwenye anga za muziki wa aina hiyo.
Rose ametoa wimbo wake huo jana Alhamisi ambao amemshirikisha mwanamuziki kutoka Kenya, Ring Tone ambaye pia huimba muziki wa aina hiyo.
Wimbo ambao umeanza kupamba chati katika baadhi ya redio za dini hapa nchini, umeonyesha kupokelewa kwa baadhi ya wasikilizaji kwa kutuma ujumbe mfupi kuomba kupigiwa kibao hicho na hata kwa baadhi ya mitaani ukipita utasikia wimbo huo unapigwa.
Kwenye wimbo huo Rose amemshukuru Mungu kwa kumvusha katika kipindi kigumu alichopitia kwani
mwaka jana mwimbaji huyo akiwa nchini Kenya alipata matatizo ya kiafya ikiwemo kukumbwa na mapepo.
Rose amewahi kutamba na nyimbo kama Mteule uwe Macho, Yesu Nakupenda, Tabu Zangu, Wambea Nao, Uko Wapi na nyingine nyingi.