Bieber atumia Sh5 bilioni kwenye hafla ya ndoa yake na Hailey Baldwin

Muktasari:

  • Bieber amekamilisha kufunga ndoa na Hailey Baldwin na kutumia Sh5 bilioni kwenye hafla ya harusi ikiwa ni mara ya pili baada ya kufunga ndoa ya awali kwenye mahakama mjini New York nchini Marekani.

Marekani. Justin Bieber na Hailey Baldwin  wafunga ndoa ya pili, mwaka mmoja baada ya kufunga ndoa kisheria katika mahakama ya New York nchini Marekani.

Bieber, 25 na Hailey, 22 wamefahamiana toka mwaka 2009 kisha kuanza uhusiano wa kimapenzi mwaka 2015 huku wakiachana na kurudiana.

Harusi na sherehe hiyo ya kifahari imefanyika South Carolina nchini Marekani na kuhudhuriwa na wageni zaidi ya 150 wakiwamo wanafamilia na watu mashuhuri ikiwamo familia ya Kardashians huku ikikadiriwa kutumia Sh5 bilioni.

Watu mashuhuri waliohudhuria ni pamoja na nyota wa Pop Katy Perry, Jaden Smith, Camilla Morrone, David Grutman na mkewe Isabela.

Bieber ametuma picha katika ukurasa wake wa Instagram alizopiga kwenye kibanda ambazo yeye na Hailey wakibusu mbele ya kamera akiwa na suti yake nyeupe wakati Hailey akionekana anang’aa na shela ya harusi.

"Nimejizawadia zawadi ya harusi" aliandika Bieber chini ya picha aliyoweka kwenye mtandao wake wa Instagram inayokadiriwa kugharimu zaidi ya dola 50,000 za Marekani.

Tovuti ya TMZ imefanikiwa kupata picha za kwanza kutoka sherehe ya harusi hiyo ambapo baadhi yake anaonekana Kylie Jenner na wengine wakicheza kwenye ukumbi kisha Justin alichukua kipaza sauti  na kuimba na wasanii wenzake .

Sherehe nzima inakadiriwa kugharimu zaidi ya Sh5 bilioni ambapo wanandoa hao wamekaa katika hoteli ya nyota tano, wametumia ndege binafsi katika safari yao ya kwenda na kurudi South Carolina na sherehe kwa ujumla.