Wimbo Gere wa Diamond, Tanasha gumzo mitandaoni

Muktasari:

Wimbo Gere wa msanii Diamond Platnumz akishirikiana mpenzi wake, Tanasha Donna umekuwa gumzo mitandaoni saa chache baada ya kuweka kipande chake katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram

Dar es Salaam. Wimbo Gere wa msanii Diamond Platnumz akishirikiana mpenzi wake, Tanasha Donna umekuwa gumzo mitandaoni saa chache baada ya kuweka kipande chake katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram.

Diamond ameuweka wimbo huo leo Jumatano Februari 19, 2020 saa 6 mchana lakini hadi saa 10:20 jioni ulikuwa umetazamwa mara 171,005.

Katika mtandao wa Youtube, wimbo huo umewekwa leo na hadi saa 10:26 ulikuwa umetazamwa mara 425,178.

Akiutambulisha wimbo huo Diamond amesema, “ninawashukuru sana kwa kuendelea kupokea kidogo niwapacho. Nyimbo hii ikawe maalum kwa ajili yako na umpendae na iwafikie wote wenye Gere na wasiopenda mahusiano yenu.”

Hii ni mara ya kwanza kwa Diamond kuimba na mpenzi wake. Katika wimbo wa Iyena, alimtumia mzazi mwenzake Zari kama mpambaji wa video ya wimbo huo aliomshirikisha Rayvanny.

Licha ya kuwa Zari ni msanii, Diamond hakuwahi kumshirikisha katika wimbo wowote.

Mbali na Zari, msanii Hamisa Mobeto ambaye pia ni mzazi mwenzake na Diamond naye hajawahi kushirikishwa katika nyimbo za msanii huyo.

Katika mtandao wa Instagram na Youtube mashabiki wa msanii huyo wamesema wimbo huo huenda ukafanya vizuri. Tanasha na Diamond wana mtoto mmoja.