Mwenyekiti baraza la Katiba Algeria ajiuzulu

Muktasari:

Ni kutokana na shinikizo la waandamanaji wanaotaka kuondolewa washirika wa Rais wa zamani, Abdulaziz Bouteflika

 Algiers ,Algeria.Mwenyekiti wa Baraza la Katiba nchini Algeria, Tayeb Belaiz amejiuzulu leo wakati maelfu ya watu wamemininika mitaani kushinikiza kuondoka kwa washirika wote wa Rais wa zamani, Abdulaziz Bouteflika.

Shirika la habari la taifa la nchi hiyo APS limeripoti kuwa Belaiz amewasilisha barua yake ya kujiuzulu kwa Rais wa mpito, Abdelkadir Bensalah.

Maandamano yameendelea tangu kujiuzulu kwa Rais Bouteflika baada ya waandamanaji kuukataa uongozi wa Bensalah, Belaiz na waziri mkuu Noureddine Bedoui.

Wanafunzi wanaendelea kuandamana kwenye mitaa ya mji mkuu Algiers wakitaka kuondoka madarakani kwa viongozi hao.

Aprili 9 Bensalah alichaguliwa na Bunge kuongoza kipindi cha mpito cha miezi mitatu kufuatia kujiuzulu kwa Rais Bouteflika kulikosababishwa na maandamano dhidi ya utawala wake wa miaka 20