Lugola atengua uteuzi wa ma-RPC watatu

Muktasari:

  • Ni wa Ilala, Temeke na Arusha wanaodaiwa kushindwa kutekeleza maagizo yake

 

Dodoma. Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola ametengua uteuzi wa makamanda wa polisi wa mikoa mitatu; Salum Hamduni (Ilala), Emmanuel Lukula (Temeke) na Ramadhani Ng'azi (Arusha).

Ametangaza uamuzi wake huo leo Jumatano Januari 16, 2019, katika mkutano na waandishi wa habari akibainisha kuwa amefanya hivyo baada ya kushauriana na vyombo anavyoviongoza.

Amesema sababu za kutengua uteuzi wa kamanda wa Ilala na Temeke ni kushindwa kusimamia mianya ya rushwa na utoaji wa dhamana kwa watuhumiwa.

Pia, amemuagiza katibu mkuu wa wizara yake kuunda kamati ambayo itapewa miezi mitatu kuchunguza vitendo vya rushwa akitaka mkazo uwekwe zaidi kwa askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani.

Waziri huyo amemtaka Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Fortunatus Muslimu kujitafakari na kujipima kama anatosha katika nafasi hiyo.